Zaburi 34

Zaburi 34

Sifa kwa wema wa Mungu

1Nitamtukuza Mwenyezi-Mungu nyakati zote,

sitaacha kamwe kuzitamka sifa zake.

2Mimi nitaona fahari juu ya Mwenyezi-Mungu,

wanyonge wasikie na kufurahi.

3Mtukuzeni Mwenyezi-Mungu pamoja nami,

sote pamoja tulisifu jina lake.

4Nilimwomba Mwenyezi-Mungu naye akanijibu,

na kuniondoa katika hofu zangu zote.

5Mgeukieni Mungu mpate kufurahi;

nanyi hamtaaibishwa kamwe.

6Maskini alimlilia Mwenyezi-Mungu, naye akamsikia,

na kumwokoa katika taabu zake zote.

7Malaika wa Mwenyezi-Mungu huwalinda wote wamchao,

na kuwaokoa katika hatari.

8Jaribuni mwone Mwenyezi-Mungu alivyo mwema.[#Taz 1Pet 2:3]

Heri mtu anayekimbilia usalama kwake.

9Mcheni Mwenyezi-Mungu enyi watakatifu wake;

maana wenye kumcha hawatindikiwi na kitu.

10Hata wanasimba hutindikiwa na kuona njaa;

lakini wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu hawakosi chochote chema.

11Njoni enyi vijana mkanisikilize,

nami nitawafundisha kumcha Mwenyezi-Mungu.

12Je, watamani kufurahia maisha,[#Taz 1Pet 3:10-12]

kuishi maisha marefu na kufurahia mema?

13Basi, acha kusema mabaya,

na kuepa kusema uongo.

14Jiepushe na uovu, utende mema;

utafute amani na kuizingatia.

15Mwenyezi-Mungu huwaangalia waadilifu,

na kusikiliza malalamiko yao;

16lakini huwapinga watu watendao maovu,

awafutilie mbali kutoka duniani.

17Waadilifu wakimlilia Mwenyezi-Mungu yeye huwasikia,

na kuwaokoa katika taabu zao zote.

18Mwenyezi-Mungu yu karibu na waliokufa moyo;

huwaokoa wote waliokata tamaa kabisa.

19Mateso ya mwadilifu ni mengi,

lakini Mwenyezi-Mungu humwokoa kutoka yote.

20Huvilinda viungo vya mwili wake wote,[#Taz Yoh 19:36]

hakuna hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa.

21Ubaya huwaletea waovu kifo;

wanaowachukia waadilifu wataadhibiwa.

22Mwenyezi-Mungu huokoa maisha ya watumishi wake,

wote wanaomkimbilia hawataadhibiwa.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania