Zaburi 6

Zaburi 6

Sala wakati wa taabu

1Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako;[#Taz Zab 38:1]

usiniadhibu kwa ghadhabu yako.

2Unihurumie, ee Mwenyezi-Mungu, nimeishiwa nguvu;

uniponye, ee Mwenyezi-Mungu, nataabika mpaka mifupani.

3Ninahangaika sana rohoni mwangu.

Ee Mwenyezi-Mungu, utakawia mpaka lini?

4Unigeukie, ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe;

unisalimishe kwa sababu ya fadhili zako.

5Huko kwa wafu hakuna anayekukumbuka;

huko kuzimu ni nani awezaye kukusifu?

6Niko hoi kwa kilio cha uchungu;

kila usiku nalowesha kitanda changu kwa machozi;

kwa kulia kwangu naulowesha mto wangu.

7Macho yangu yamechoka kwa huzuni;

yamefifia kwa kutaabishwa na adui.

8Ondokeni kwangu enyi nyote watenda maovu![#Taz Mat 7:23; Luka 13:27]

Maana Mwenyezi-Mungu amesikia kilio changu.

9Mwenyezi-Mungu amesikia ombi langu;

Mwenyezi-Mungu amekubali sala yangu.

10Maadui zangu wote wataaibika na kufadhaika;

watarudi nyuma na kuaibishwa ghafla.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania