The chat will start when you send the first message.
1Basi, ikiwa mmefufuka pamoja na Kristo, panieni mambo ya juu, kule Kristo aliko, ameketi upande wa kulia wa Mungu.[#3:1-3 Kol 2:12; rejea Rom 6:13-14.; #3:1 Zab 110:1 ambayo imenukuliwa pia katika Mat 22:44; Mate 2:34; rejea Efe 1:20; 2:6; Ebr 1:3.]
2Muwe na hamu ya mambo ya huko juu, na siyo mambo ya hapa duniani.
3Maana nyinyi mmekufa na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu.[#3:3 Si rahisi kuelewa anachosema Paulo hapa, ila ni kwamba maana ya maisha kamili ya mwaamini yaani mtu anayemwamini Kristo, itadhihirika wakati ule Kristo atakapofunuliwa, yaani wakati wa kurudi kwake (aya ya 4); mpaka wakati huo hali kamili ya mwaamini itakuwa imefichwa kwa Mungu. (“Kwa Mungu” katika barua za Paulo yanatumika hapa, katika 1Thes 1:1 na 2Thes 1:1). Maneno anayosema Paulo mwishoni mwa kifungu hiki, aya ya 3 na 4, yanapatana na maelezo haya.]
4Uhai wenu halisi ni Kristo, na wakati atakapotokea ndipo nanyi pia mtakapotokea pamoja naye katika utukufu.[#3:4 Au, “Kristo ndiye uhai wetu”. Gal 2:20; Fil 2:1; rejea pia Fil 3:21; 1Yoh 3:2.]
5Basi, ueni chochote kilicho ndani yenu ambacho ni cha kidunia: uasherati, uchafu, shauku, tamaa mbaya na uchu (ambao ni sawa na kuabudu sanamu).[#3:5,8 Katika aya hizi mbili kuna orodha ya vitendo vibaya, vitano vitano katika kila aya. Na kama vile kuonesha kinyume cha vitendo hivyo vibaya, katika aya ya 12 tunapewa orodha ya vitendo vizuri, navyo ni vitano pia. Taz Rom 1:29-32 maelezo.]
6Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya Mungu huwajia wote wanaomwasi.
7Wakati mmoja nyinyi pia mliishi kufuatana na mambo hayo, mlipotawaliwa nayo.
8Lakini sasa mnapaswa kuachana na mambo haya yote: hasira, tamaa na uovu; kufuru au maneno yasiyofaa yasitoke kamwe vinywani mwenu.
9Msiambiane uongo, kwani nyinyi mmekwisha vua ule utu wa kale pamoja na matendo yake yote,
10mkavaa utu mpya. Huu unaendelea kurekebishwa na Mungu, Muumba wake, kadiri ya mfano wake, ili mpate kumjua Mungu kwa ukamilifu.[#3:9-10 Taz Efe 4:24 maelezo; rejea Kol 2:11 na Rom 6, ambapo Paulo anashughulikia wazo hilo la utu mpya kwa mapana zaidi.; #3:10 Yaani mfano wake Mungu: Mwa 1:26; rejea 2Kor 5:17; Gal 6:15; Efe 2:10.]
11Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote.[#3:11 Rom 10:12; 1Kor 12:13; Gal 3:28.]
12Nyinyi ni watu wake Mungu; yeye aliwapenda na kuwateua. Kwa hiyo, basi, vaeni moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu.[#3:12-15 Rejea maelezo ya maisha kulingana na Roho katika Gal 5:22-23.]
13Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu analo jambo lolote dhidi ya mwenzake. Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe nyinyi.
14Zaidi ya hayo yote, zingatieni upendo, kwani upendo huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili.
15Nayo amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu; maana kwa ajili hiyo nyinyi mmeitwa katika mwili huo mmoja. Tena muwe na shukrani![#3:15 Rejea Yoh 14:27; Efe 2:14; Fil 4:7.]
16Ujumbe wa Kristo na ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni Zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani.[#3:16-17 Efe 5:19-20; taz Kol 1:15-20 maelezo.]
17Na, kila mfanyacho kwa neno au tendo, fanyeni vyote kwa jina la Bwana Yesu na kumshukuru Mungu Baba kwa njia yake.
18Enyi wake, watiini waume zenu, kwani ndivyo apendavyo Bwana.[#3:18-19 Taz Efe 5:23-24, maelezo.]
19Nanyi waume, wapendeni wake zenu, na msiwe wakali kwao.
20Enyi watoto, watiini wazazi wenu daima maana hiyo humpendeza Bwana.
21Nanyi wazazi, msiwachukize watoto wenu, la sivyo watakata tamaa.
22Enyi watumwa, watiini wakuu wenu wa kidunia katika mambo yote, na si tu wakati wanapowatazama kwa kuwa mnataka kujipendekeza kwao; ila fanyeni hivyo kwa moyo wote, kwa sababu ya kumcha Bwana.[#3:22 Utumwa ulikuwa jambo la kawaida nyakati hizo za kale. A.J. linafundisha kwamba, kwa sababu ya Kristo (katika Kristo) si kitu kuwa mtu huru au mtumwa (Gal 3:28; Efe 6:8; Kol 3:11), na kwamba sote tunapaswa kutumikia kwa upendo (rejea Mat 20:25-28 na sambamba zake). Hapa, watumwa wanahimizwa watumikie kwa uaminifu; na hao wakuu wao wanapaswa kuwatendea watumwa wao kwa uadilifu na haki. Rejea pia Efe 6:5-9; 1Tim 6:1-2; Tito 2:9-10; 1Pet 2:18-25.]
23Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu.
24Kumbukeni kwamba atawapeni tuzo lile alilowawekea watu wake. Mtumikieni Kristo Bwana!
25Atendaye mabaya atalipwa kufuatana na ubaya wake; Mungu hana ubaguzi.