Isaya 18

Isaya 18

Mungu ataiadhibu Kushi

1Ole, wake nchi iliyojaa mvumo wa mabawa,[#18:1 Yamkini yahusu wingi wa wadudu ambao kwa kawaida walikuwako kwa wingi katika eneo hilo lililokuwa na maji mengi ya mto Nili. Kuhusu jina “Kushi” taz 11:11. Hapa jina hilo laweza kumaanisha Ethiopia au Nubia (Sudani).]

nchi iliyoko ng'ambo ya mito ya Kushi!

2Inatuma wajumbe ambao wanasafiri mtoni Nili,

wamepanda mashua za mafunjo.

Nendeni, enyi wajumbe wepesi,

kwa taifa kubwa na hodari,

la watu warefu na wa ngozi laini.

Watu hao wanaoogopwa kila mahali

na nchi yao imegawanywa na mito.

3Enyi wakazi wote ulimwenguni,

nanyi mkaao duniani!

Ishara itakapotolewa mlimani, tazameni!

Tarumbeta itakapopigwa, sikilizeni.

4Maana, Mwenyezi-Mungu ameniambia hivi:

“Toka makao yangu juu nitatazama yanayotukia,

nimetulia kama joto katika mwanga wa jua,

kama wingu la umande wakati wa mavuno.

5Maana, kabla ya mavuno,

wakati wa kuchanua umekwisha,

maua yamepukutika na kuwa zabibu mbivu,

Mungu atakata chipukizi kwa kisu cha kupogolea,

na kuyakwanyua matawi yanayotanda.

6Yote yataachiwa ndege milimani,

na wanyama wengine wa porini.

Ndege walao nyama watakaa humo

wakati wa majira ya kiangazi,

na wanyama wa porini watafanya makao humo

wakati wa majira ya baridi.”

7Wakati huo, Mwenyezi-Mungu wa majeshi ataletewa tambiko kutoka kwa watu warefu wenye ngozi laini, watu watishao karibu na mbali, taifa la watu wenye nguvu na ushindi, ambalo ardhi yake imegawanywa na mito. Ataletewa tambiko hizo mlimani Siyoni anapoabudiwa yeye Mwenyezi-Mungu wa majeshi.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania