The chat will start when you send the first message.
1Wakati huo, Yudithi alisikia mambo yaliyotokea. Yeye alikuwa binti wa Merari, mwana wa Oksi, mwana wa Yosefu, mwana wa Ozieli, mwana wa Elkia, mwana wa Anania, mwana wa Gideoni, mwana wa Refaimu, mwana wa Ahitubu, mwana wa Elia, mwana wa Hilkia, mwana wa Eliabu, mwana wa Nathanaeli, mwana wa Salamieli, mwana wa Sarasadai, mwana wa Israeli.[#8:1 Tangu hapa na kuendelea, mhusika mkuu katika simulizi hili atakuwa Yudithi. Jina hili lina maana ya “Myahudi”.]
2Manase, mume wa Yudithi, ambaye alikuwa wa kabila la mkewe na wa ukoo mmoja, alikuwa amefariki wakati wa mavuno ya shayiri.[#8:2 Ingawa hapa haisemwi moja kwa moja na kwa uwazi, baadaye (9:2) atatajwa Simeoni ili kumtambulisha Yudithi kwamba alikuwa wa kabila la Simeoni. Rejea Hes 1:6.]
3Alikuwa amepigwa sana na jua alipokuwa shambani akisimamia wafanyakazi wakifunga miganda. Baadaye alikwenda akalala kitandani. Halafu alifia katika mji wake Bethulia. Alizikwa katika kaburi la ukoo wake, kati ya mji wa Dothani na mji wa Balamoni.
4Kwa muda wa miaka mitatu na miezi minne, Yudithi aliishi akiwa mjane.[#8:4 Hali ya Yudithi ya kuwa mjane iliongezea unyonge wake, unyonge ambao ni mfano wa hali ya Wayahudi.]
5Katika muda huo wa huzuni, yeye mwenyewe alipiga hema darini mwa nyumba yake na kukaa humo, amefunga kiunoni mavazi ya gunia na kuvaa mavazi ya ujane.[#8:5 Kuvaa mavazi ya gunia ilikuwa njia mojawapo ya kuonesha uchungu na mateso.]
6Katika muda huo wote wa ujane wake, alifunga, isipokuwa jioni ya kuanza Sabato, Sabato yenyewe, jioni ya sikukuu ya mwezi mwandamo na sikukuu yenyewe, pamoja na sikukuu zote na siku za mapumziko ambazo Waisraeli waliziadhimisha.
7Yudithi alikuwa mwanamke mzuri sana. Marehemu Manase, mumewe, alikuwa amemwachia dhahabu, fedha, watumishi na watumwa wa kiume na kike, mifugo na shamba na alitunza mali yake yote.
8Hakuna mtu aliyekuwa na neno dhidi yake, kwani alimcha Mungu kwa dhati.
9Yudithi aliposikia maji yalivyowafanya watu wateseke na jinsi walivyokuwa wanalalamika vikali dhidi ya viongozi wa mji na jinsi Uzia alivyowaambia na kuwaapia kutoa mji kwa Waashuru baada ya siku tano,
10Yudithi alimtuma mara moja mjakazi wake aliyekuwa mkuu nyumbani mwake, ili kuwaita Kabrisi, Karmisi na wazee wa mji.
11Walipomjia, Yudithi aliwaambia, “Nisikilizeni viongozi wa Bethulia. Mlikosea kuzungumza na watu kama mlivyofanya leo na kujifunga kwa kiapo, kwa kumwasi Mungu, kusalimisha mji kwa maadui zetu ikiwa Bwana hakuwapatia msaada katika muda huo uliopangwa.
12Nyinyi ni nani hata kumjaribu Mungu kama mlivyofanya leo, na kujitia mahali pa Mungu kuhusu mambo ya watu?[#8:12-13 Hao viongozi walitazamia kwamba Mungu, kwa wakati maalumu, angefanya muujiza kuwaokoa. Hiyo ilikuwa kama kumsukuma Mungu (rejea Kumb 6:16).]
13Mnamjaribu Bwana Mwenye Nguvu! Hamfahamu lolote, wala hamtafahamu.
14Kama hamwezi kuyafahamu yaliyo moyoni mwa mwanaadamu, wala anayofikiri, mnawezaje basi, kufahamu akili ya Mungu aliyeumba vitu vyote au kuyaelewa mawazo yake au makusudi yake? Sivyo hivyo ndugu! Msimkasirishe Bwana Mungu wetu!
15Ikiwa hataki kutusaidia katika muda huu wa siku tano, bado anaweza kutukinga na hatari kwa siku nyingi jinsi yeye apendavyo, kama alivyo na uwezo wa kutuangamiza mbele ya maadui zetu.
16Hamna haki ya kudai uhakikisho pale mipango ya Mungu inapohusika. Mungu hastahili kutishwa wala hapaswi kufanyiwa mzaha, kama mwanaadamu wa kawaida.
17Zaidi ya hayo! Kama tumngojeavyo atukomboe, basi tumsihi atusaidie; ikiwa hayo ni mapenzi yake, atakisikiliza kilio chetu.
18Kamwe katika nyakati zetu hizi na hata leo; hakuna kabila moja miongoni mwa makabila yetu au jamaa au kijiji kinachoiabudu miungu iliyofanywa kwa mikono ya mwanadamu, kama hapo awali.
19Ndiyo maana wazee wetu waliachwa wauawe kwa upanga na kutekwa, halafu waliangamia katika taabu kwa kushambuliwa na maadui zetu.
20Sisi kwa upande wetu hatumwabudu mungu yeyote mwingine bali yeye; kwa hiyo tuwe na tumaini kuwa hatatuchukia wala kulitupilia mbali taifa letu.
21“Ikiwa kweli watatuteka, basi, eneo zima la Yudea litatekwa pia, hata mahali petu patakatifu patabomolewa, nasi tutalipa kwa damu yetu kwa ajili ya tendo lao la kufuru.
22Kuuawa kwa ndugu zetu, kutekwa kwa nchi yetu, na kuangamizwa urithi wetu vitakuwa lawama yetu wenyewe kati ya mataifa tutakaokuwa watumwa wao; nao mabwana zetu wapya watatudharau kama taifa ovu na lenye hila.
23Hakuna jema litakalopatikana kutokana na utumwa wetu, bali Bwana Mungu wetu ataufanya kuwa jambo la aibu.
24“Sasa ndugu zangu, ni lazima sisi tuwe mfano kwa ndugu zetu, maana maisha yao yanatutegemea sisi, kadhalika mahali patakatifu: hekalu na madhabahu ni juu yetu kuvitunza.[#8:24 Kiini cha msimamo mpya unaotakiwa na Yudithi ni kule kujihisi kwamba wao ni kitu kimoja na hekalu la Mungu na taifa lote.]
25Zaidi ya hayo yatupasa kumshukuru Bwana Mungu wetu ambaye kama alivyowajaribu wazee wetu ndivyo anavyotujaribu.
26Kumbukeni jinsi alivyomtendea Abrahamu majaribu yote kuhusu Isaka, na yale yaliyompata Yakobo alipomtumikia Labani, mjomba wake, katika nchi ya Mesopotamia ya Siria.
27Maana kama majaribu hayo yalikusudiwa na Mungu ili kuchunguza mioyo yao, hivyo basi hiki si kisasi ambacho Mungu anatulipiza, bali, ni onyo ambalo limepelekwa na Bwana kwa wale anaowapenda.”[#8:27 Kuhusu fundisho au kupata nidhamu kama faida inayopatikana kutoka mateso, rejea Yobu 5:17-18; Meth 3:11-12; 2Mak 6:12-16; Ebr 12:4-11.]
28Kisha Uzia alimwambia Yudithi, “Yote uliyosema yanatokana na moyo safi, na hakuna awezaye kupinga neno lolote.
29Leo si mara ya kwanza kwako kutuonesha hekima yako. Tangu utoto wako, sisi tumetambua ulivyo mwenye akili na moyo thabiti.
30Lakini kwa ajili ya kuona kiu sana watu wetu walitushurutisha kufanya kama tulivyowaahidi na kujifunga kwa kiapo halisi.
31Wewe ni mcha Mungu sana, mwombe Bwana atuletee mvua ili visima vyetu viwe na maji, ili kuangamia kwetu kukome.”[#8:31 Hata hivyo, hao viongozi wanafikiri kwamba Mungu anachukua hatua moja kwa moja kwa tukio la mvua.]
32Basi, Yudithi akawaambia, “Nisikilizeni, ninakusudia kutenda jambo ambalo litakumbukwa katika vizazi vyote vya wazawa wetu.
33Leo usiku, shika ulinzi kwenye lango la mji. Mimi na mjakazi wangu tutatoka mjini. Kabla haijafika siku ile ambayo umeahidi kusalimisha mji wetu kwa maadui zetu haijafika, Bwana atanitumia mimi kuwaokoa Waisraeli.
34Lakini msiniulize ninalokusudia kutenda; sitawaambieni mpaka nitakapolitenda.”
35Uzia pamoja na wakuu wakamwambia, “Nenda kwa amani! Bwana Mungu akuongoze kuwalipiza kisasi maadui zetu”.
36Hivyo, wakaondoka kutoka kwenye kibanda kilichokuwa darini, wakarudi kwao.