Zaburi 12

Zaburi 12

Kuomba msaada

1Fanya haraka, ee Mwenyezi-Mungu!

Watu wema wamekwisha;

waaminifu wametoweka miongoni mwa watu.

2Kila mmoja humdanganya mwenzake,

husema kwa kudanganya na kwa moyo wa unafiki.

3Ee Mwenyezi-Mungu

uikomeshe hiyo midomo ya udanganyifu,

na ndimi hizo zinazojigamba kupindukia.

4Wao husema: “Kwa ndimi zetu tutashinda;

midomo tunayo, nani awezaye kututawala?”

5Lakini Mwenyezi-Mungu asema:

“Kwa sababu maskini wanadhulumiwa,

na wahitaji wanapiga kite, sasa naja,

nami nitawapa usalama wanaoutazamia.”

6Neno la Mwenyezi-Mungu ni safi,

safi kama fedha iliyosafishwa katika tanuri,

naam, kama fedha iliyosafishwa mara saba.

7Utulinde, ee Mwenyezi-Mungu,

utukinge daima na kizazi hiki kiovu.

8Waovu wanazunguka kila mahali;

upotovu unatukuzwa kati ya watu.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania