Hosea 2

Hosea 2

1“Waambie ndugu zako, ‘Watu wangu,’ na pia waambie dada zako, ‘Wapendwa wangu.’

Israeli kuadhibiwa na kurudishwa

2“Mkemeeni mama yenu, mkemeeni,

kwa maana yeye si mke wangu,

nami si mume wake.

Aondoe sura ya uzinzi katika uso wake

na uzinzi kati ya matiti yake.

3Kama sivyo nitamvua nguo zake awe uchi

na kumwacha uchi kama siku ile aliyozaliwa.

Nitamfanya kama jangwa,

nitamgeuza awe nchi ya kiu,

nami nitamuua kwa kiu.

4Sitaonesha upendo wangu kwa watoto wake,

kwa sababu ni watoto wa uzinzi.

5Mama yao amekosa uaminifu

na amewachukua mimba katika aibu.

Gomeri alisema, ‘Nitawaendea wapenzi wangu,

ambao hunipa chakula changu

na maji yangu,

sufu yangu na kitani yangu, mafuta yangu

na kinywaji changu.’

6Kwa hiyo mimi Mungu nitaizuia njia yake

kwa vichaka vya miiba,

nitamjengea ukuta ili

asiweze kutoka.

7Gomeri atawafuatia wapenzi wake lakini hatawapata;

atawatafuta lakini hatawapata.

Kisha atasema,

‘Nitarudi kwa mume wangu kama kwanza,

kwa maana nilikuwa na hali njema

kuliko sasa.’

8Gomeri hajakubali kuwa mimi ndiye

niliyempa nafaka, divai mpya na mafuta,

niliyemwongezea fedha na dhahabu waliyoitumia

kwa kumtumikia Baali.

9“Kwa hiyo nitachukua nafaka yangu wakati itakapokomaa

na divai yangu mpya wakati itakapokuwa tayari.

Nitamnyangʼanya sufu yangu na kitani yangu

iliyokusudiwa kufunika uchi wake.

10Basi sasa nitaufunua ufisadi wake

mbele ya wapenzi wake;

hakuna yeyote atakayemtoa

mikononi mwangu.

11Nitakomesha furaha na macheko yake yote:

sikukuu zake za mwaka,

sikukuu za Miandamo ya Mwezi,

siku zake za Sabato,

sikukuu zake zote zilizoamriwa.

12Nitaiharibu mizabibu yake na mitini yake,

ambayo alisema yalikuwa malipo yake

kutoka kwa wapenzi wake;

nitaifanya kuwa kichaka,

nao wanyama pori wataila.

13Nitamwadhibu kwa ajili ya siku

alizowafukizia uvumba Mabaali;

alipojipamba kwa pete

na kwa vito vya thamani,

na kuwaendea wapenzi wake,

lakini mimi alinisahau,”

asema Bwana .

14“Kwa hiyo sasa nitamshawishi;

nitamwongoza hadi jangwani

na kuzungumza naye kwa upole.

15Huko nitamrudishia mashamba yake ya mizabibu,

nami nitalifanya Bonde la Akori

mlango wa matumaini.

Huko ataimba kama alivyofanya katika siku za ujana wake,

kama siku zile alizotoka Misri.

16“Katika siku ile,” asema Bwana ,

“utaniita mimi ‘Mume wangu’;

hutaniita tena mimi ‘Bwana wangu.’

17Nitaondoa majina ya Mabaali kutoka mdomoni mwake,

wala hataomba tena kwa majina yao.

18Katika siku ile nitafanya agano kwa ajili yao

na wanyama wa kondeni, na ndege wa angani,

na viumbe vinavyotambaa ardhini.

Upinde, upanga na vita,

nitaondolea mbali katika nchi,

ili wote waweze kukaa salama.

19Nitakuposa uwe wangu milele;

nitakuposa kwa uadilifu na haki,

kwa upendo na huruma.

20Nitakuposa kwa uaminifu,

nawe utamkubali Bwana .

21“Katika siku ile nitajibu,”

asema Bwana ,

“nitajibu kwa anga,

nazo anga zitajibu kwa nchi;

22nayo nchi itajibu kwa nafaka,

divai mpya na mafuta,

navyo vitajibu kwa Yezreeli.

23Nitampanda katika nchi kwa ajili yangu mwenyewe;

nami nitaonesha pendo langu kwake

yule ambaye nilimwita, ‘Si Mpendwa Wangu.’

Nitawaambia wale walioitwa, ‘Sio Watu Wangu,’

‘Ninyi ni Watu Wangu’;

nao watasema, ‘Wewe ndiwe Mungu wangu’.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.