Hosea 4

Hosea 4

Shtaka dhidi ya Israeli

1Sikieni neno la Bwana , enyi Waisraeli,

kwa sababu Bwana analo shtaka

dhidi yenu ninyi mnaoishi katika nchi:

“Hakuna uaminifu, hakuna upendo,

hakuna kumjua Mungu katika nchi.

2Kuna kulaani tu, uongo na uuaji,

wizi na uzinzi,

bila kuwa na mipaka,

nao umwagaji damu mmoja

baada ya mwingine.

3Kwa sababu hii nchi huomboleza,

wote wanaoishi ndani yake wanadhoofika;

wanyama wa kondeni, ndege wa angani

na samaki wa baharini wanakufa.

4“Lakini mtu yeyote na asilete shtaka,

mtu yeyote na asimlaumu mwenzake,

kwa maana watu wako ni kama wale

waletao mashtaka dhidi ya kuhani.

5Unajikwaa usiku na mchana,

nao manabii hujikwaa pamoja nawe.

Kwa hiyo nitamwangamiza mama yako:

6watu wangu wanaangamizwa

kwa kukosa maarifa.

“Kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa,

mimi nami nitakukataa wewe

usiwe kuhani kwangu mimi;

kwa kuwa umeacha kuijali sheria ya Mungu wako

mimi nami sitawajali watoto wako.

7Kadiri makuhani walivyoongezeka,

ndivyo walivyozidi kutenda dhambi dhidi yangu,

walibadilisha utukufu wao kwa kitu cha aibu.

8Wanajilisha dhambi za watu wangu

na kupendezwa na uovu wao.

9Hata itakuwa: Kama walivyo watu,

ndivyo walivyo makuhani.

Nitawaadhibu wote wawili kwa ajili ya njia zao

na kuwalipa kwa matendo yao.

10“Watakula lakini hawatashiba;

watajiingiza katika ukahaba

lakini hawataongezeka,

kwa sababu wamemwacha Bwana

na kujiingiza wenyewe

11katika ukahaba;

kunywa divai ya zamani na divai mpya

huondoa ufahamu

12wa watu wangu.

Hutaka shauri kutoka kwa sanamu ya mti

nao hujibiwa na fimbo ya mti.

Roho ya ukahaba imewapotosha,

hawana uaminifu kwa Mungu wao.

13Wanatoa dhabihu juu ya vilele vya milima

na sadaka za kuteketezwa juu ya vilima,

chini ya mialoni, milibua na miela,

ambako kuna vivuli vizuri.

Kwa hiyo binti zenu wamegeukia ukahaba

na wake za wana wenu uzinzi.

14“Sitawaadhibu binti zenu wakati

wanapogeukia ukahaba,

wala wake za wana wenu

wanapofanya uzinzi,

kwa sababu wanaume wenyewe huandamana na malaya

na kutambikia pamoja na makahaba

wa mahali pa ibada za sanamu:

watu wasiokuwa na ufahamu

wataangamia!

15“Ingawa umefanya uzinzi, ee Israeli,

Yuda naye asije akawa na hatia.

“Usiende Gilgali,

usipande kwenda Beth-Aveni.

Wala usiape,

‘Hakika kama Bwana aishivyo!’

16Waisraeli ni wakaidi,

kama ndama jike mkaidi.

Ni jinsi gani basi Bwana anaweza kuwachunga

kama wana-kondoo

katika shamba la majani?

17Efraimu amejiunga na sanamu,

achana naye!

18Hata wakati wamemaliza vileo vyao

wanaendelea na ukahaba wao,

watawala wao hupenda sana

njia za aibu.

19Kisulisuli kitawafagilia mbali

na dhabihu zao zitawaletea aibu.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.