Wimbo 5

Wimbo 5

1Nimekuja kwenye bustani yangu, dada yangu,

bibi arusi wangu;

nimekusanya manemane yangu pamoja

na manukato yangu.

Nimekula sega langu la asali na asali yangu;

nimekunywa divai yangu na maziwa yangu.

Kuleni, enyi rafiki, mnywe;

kunyweni ya kutosha, ee wapenzi.

2Nililala lakini moyo wangu ulikuwa macho.

Sikiliza! Mpenzi wangu anabisha:

“Nifungulie, dada yangu, mpendwa wangu,

hua wangu, usiye na hitilafu.

Kichwa changu kimeloa umande,

na nywele zangu manyunyu ya usiku.”

3Nimevua joho langu:

je, ni lazima nivae tena?

Nimenawa miguu yangu:

je, ni lazima niichafue tena?

4Mpenzi wangu aliweka mkono wake kwenye tundu la komeo;

moyo wangu ulianza kugonga kwa ajili yake.

5Niliinuka kumfungulia mpenzi wangu,

mikono yangu ikidondosha manemane,

vidole vyangu vikitiririka manemane,

penye vipini vya komeo.

6Nilimfungulia mpenzi wangu,

lakini mpenzi wangu alishaondoka;

alikuwa ameenda zake.

Moyo wangu ulishuka kwa kuondoka kwake.

Nilimtafuta lakini sikumpata.

Nilimwita lakini hakunijibu.

7Walinzi walinikuta

walipokuwa wakifanya zamu za ulinzi mjini.

Walinipiga, wakanijeruhi,

wakaninyangʼanya joho langu,

hao walinzi wa kuta!

8Enyi binti za Yerusalemu, ninawaagiza:

mkimpata mpenzi wangu,

mtamwambia nini?

Mwambieni ninazimia kwa mapenzi.

9Je, mpenzi wako ni bora kuliko wengine namna gani,

wewe uliye mzuri kupita wanawake wote?

Je, mpenzi wako ni mzuri kuliko wengine, namna gani,

hata unatuagiza hivyo?

10Mpenzi wangu anangʼaa, tena ni mwekundu,

wa kuvutia miongoni mwa wanaume kumi elfu.

11Kichwa chake ni dhahabu safi kuliko zote,

nywele zake ni za mawimbi

na ni nyeusi kama kunguru.

12Macho yake ni kama ya hua

kandokando ya vijito vya maji,

aliyeogeshwa kwenye maziwa,

yaliyopangwa kama vito vya thamani.

13Mashavu yake ni kama matuta

ya mimea ya manukato.

Midomo yake ni kama yungiyungi

inayodondosha manemane.

14Mikono yake ni fimbo za dhahabu

iliyopambwa kwa krisolitho.

Mwili wake ni kama pembe ya ndovu iliyongʼarishwa

iliyopambwa na yakuti samawi.

15Miguu yake ni nguzo za marumaru

zilizosimikwa katika vitako vya dhahabu safi.

Sura yake ni kama Lebanoni,

bora kama miti yake ya mierezi.

16Kinywa chake chenyewe ni utamu,

kwa ujumla yeye ni wa kupendeza.

Huyu ndiye mpenzi wangu, huyu ndiye rafiki yangu,

ee binti za Yerusalemu.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.