Zaburi 143

Zaburi 143

Sala ya ukombozi kutoka kwa adui

1Ee BWANA, uisikie sala yangu, uzisikilize dua zangu Unijibu Kwa uaminifu wako,

Unijibu kwa haki yako.

2Wala usimhukumu mtumishi wako,[#Ayu 14:3; 4:17; Mhu 7:20; Rum 3:20; Gal 2:16]

Maana kwako hakuna aliye hai mwenye haki.

3Maana adui ameifuatia nafsi yangu,[#Zab 7:1-2]

Ameutupa chini uzima wangu.

Amenikalisha mahali penye giza,

Kama watu waliokufa zamani.

4Na roho yangu imezimia ndani yangu,[#Zab 61:2]

Moyo wangu ndani yangu umeshtuka.

5Nimezikumbuka siku za kale,[#Zab 77:5,11]

Nimeyatafakari matendo yako yote,

Naziwaza kazi za mikono yako.

6Nakunyoshea mikono yangu;[#Zab 28:2]

Nafsi yangu inakuonea kiu kama nchi kame.

7Ee BWANA, unijibu hima, roho yangu imelegea;

Usinifiche uso wako,

Nisifanane nao washukao shimoni.

8Uniwezeshe kusikia fadhili zako asubuhi,

Kwa maana nimekutumaini Wewe.

Unifundishe njia nitakayoiendea,

Kwa maana ninakuinulia nafsi yangu.

9Ee BWANA, uniponye na adui zangu;

Nimekukimbilia Wewe, unifiche.

10Unifundishe kuyatenda mapenzi yako,[#Zab 25:4; Yn 14:26; Rum 5:5; Efe 4:30; Gal 5:22-23]

Kwa maana ndiwe Mungu wangu;

Roho yako mwema aniongoze katika njia iliyo sawa,

11Ee BWANA, uniponye kwa ajili ya jina lako,

Kwa haki yako unitoe roho yangu taabuni;

12Kwa fadhili zako utawakatilia mbali adui zangu;

Na kuwaangamiza wote wanitesao nafsi,

Kwa maana mimi ni mtumishi wako.

The Holy Bible in Kiswahili, Revised Union Version © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 2013. 
Published by: Bible Society of Tanzania