Mwanzo 9

Mwanzo 9

Agano la Mungu na Nuhu

1Mungu akambariki Nuhu na wanawe, akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.[#Mwa 1:28]

2Kila mnyama wa nchi atawaogopa ninyi na kuwahofu, na kila ndege wa angani: pamoja na vitu vyote vilivyojaa katika ardhi, na samaki wote wa baharini; vimetiwa mikononi mwenu.[#Hos 2:18; Yak 3:7]

3Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapa hivi vyote.[#Kum 12:15; 14:3]

4Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile.[#1 Sam 14:34; Mdo 15:20,29; Law 7:26-27; 17:10-14; 19:26; Kum 12:16,23; 15:23]

5Hakika damu yenu ya uhai wenu nitaitaka; na kwa mkono wa kila mnyama nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa ndugu ya mtu nitataka uhai wa mwanadamu.[#Kut 21:28,29; Hes 35:31; Mdo 17:26]

6Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu, maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu.[#Kut 21:12,14; Law 24:17; Mt 26:52; Ufu 13:10; 1 Kor 11:7; Mwa 1:26; Kut 20:13]

7Nanyi zaeni, mkaongezeke; zaeni sana katika nchi, mkaongezeke ndani yake.[#Mwa 1:28]

8Mungu akamwambia Nuhu, na wanawe pamoja naye, akisema,

9Tazama, nilithibitisha agano langu nanyi; tena na uzao wenu baada yenu;

10tena na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, ndege, na mnyama wa kufugwa, na kila mnyama wa mwitu katika nchi pamoja nanyi; wote wanaotoka katika safina, hata kila kilicho hai katika nchi.[#Mwa 8:1]

11Na agano langu nitalithibitisha nanyi; wala kila chenye mwili hakitafutwa tena kwa maji ya gharika; wala hakutakuwa tena gharika, baada ya hayo, kuiharibu nchi.[#2 Pet 3:5]

12Mungu akasema, Hii ndiyo ishara ya agano nifanyalo kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, kwa vizazi vyote hata milele;[#Mt 26:26-28]

13Mimi nauweka upinde wangu winguni, nao utakuwa ni ishara ya agano kati yangu na nchi.

14Hata itakuwa nikitanda mawingu juu ya nchi, upinde utaonekana winguni,

15nami nitalikumbuka agano langu, lililoko kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili, wala maji hayatakuwa gharika tena kuwaharibu wote wenye mwili.[#Kut 28:12; Law 26:42,45; Eze 16:60; Isa 54:9]

16Basi huo upinde utakuwa winguni; nami nitauangalia nipate kulikumbuka agano la milele lililoko kati ya Mungu na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili kilichoko katika nchi.[#Mwa 17:13,19; 2 Sam 23:5]

17Mungu akamwambia Nuhu, Hii ndiyo ishara ya agano nililoliweka kati yangu na watu wote walioko katika nchi.

Nuhu na wanawe

18Wana wa Nuhu waliotoka katika safina, ni Shemu, na Hamu, na Yafethi; na Hamu ndiye baba wa Kanaani.[#Mwa 10:6]

19Hawa watatu walikuwa wana wa Nuhu na kwa hao nchi yote ikaenea watu.[#Mwa 10:32; 1 Nya 1:4]

20Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu;[#Mwa 3:19; 4:2; Mhu 5:9]

21akanywa divai, akalewa; akawa uchi katika hema yake.[#Mwa 19:32,36; Mit 20:1; Efe 5:18]

22Hamu, baba wa Kanaani, akauona uchi wa baba yake, akawaeleza ndugu zake wawili waliokuwa nje.

23Shemu na Yafethi wakatwaa vazi, wakalitanda mabegani mwao wote wawili, wakaenda kinyumenyume, wakaufunika uchi wa baba yao; na nyuso zao zilielekea nyuma, wala hawakuuona uchi wa baba yao.[#Kut 20:12; Gal 6:1]

24Nuhu akalevuka katika ulevi wake, akajua mwana wake mdogo alivyomtendea.

25Akasema,[#Kum 27:16; Mt 25:41; Yos 9:23; 1 Fal 9:20]

Na alaaniwe Kanaani;

Atakuwa mtumwa kabisa kwa ndugu zake.

26Akasema,[#Zab 144:15; Ebr 11:16]

Na atukuzwe BWANA Mungu wa Shemu;

Na Kanaani awe mtumwa wake.

27Mungu amwongezee Yafethi.[#Efe 2:13,14; 3:6]

Na akae katika hema za Shemu;

Na Kanaani awe mtumwa wake.

28Na Nuhu akaishi baada ya ile gharika miaka mia tatu na hamsini.

29Siku zote za Nuhu zilikuwa miaka mia tisa na hamsini, akafa.[#Mwa 3:19; Ayu 30:23; 34:15; Zab 89:48; Rum 5:12; 1 Kor 15:21; Ebr 9:27]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya