Zaburi 42

Zaburi 42

KITABU CHA PILI

Sala ya Mkimbizi

1Kama paa atamanivyo maji ya kijito,

ndivyo ninavyokutamani, ee Mungu wangu!

2Naona kiu ya Mungu, kiu ya Mungu aliye hai.

Nitafika lini kwake na kuuona uso wake?

3Machozi yamekuwa chakula changu mchana na usiku,

waliponiambia kila siku: “Yuko wapi Mungu Wako!”

4Nakumbuka tena mambo haya

kwa majonzi moyoni mwangu:

Jinsi nilivyokwenda na umati wa watu,

nikawaongoza kwenda nyumbani kwa Mungu

wakipiga vigelegele vya shukrani;

umati wa watu wakifanya sherehe!

5Mbona nasononeka hivyo moyoni?

Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu?

Nitamtumainia Mungu,

maana nitamsifu tena

yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.

6Nimesongwa na huzuni moyoni mwangu,

kwa hiyo ninakukumbuka wewe, ee Mungu,

kutoka katika eneo la Yordani,

kutoka mlima Hermoni na Mizari.

7Nimeporomoshewa mafuriko ya maji

mafuriko ya maji yaja karibu

nayo yaita maporomoko mapya.

Mawimbi na mapigo yako yamenikumba.

8Mwenyezi-Mungu atanijalia fadhili zake mchana;

nami nimwimbie wimbo wa sifa usiku,

nimwombe Mungu anipaye uhai.

9Namwambia Mungu, mwamba wangu:

“Kwa nini umenisahau?

Yanini niende huko na huko nikiomboleza

kwa kudhulumiwa na adui yangu?”

10Nimepondwa kwa matukano yao,

wanaponiuliza kila siku:

“Yuko wapi, Mungu wako!”

11Mbona nasononeka hivyo moyoni?

Kwa nini nahangaika hivyo?

Nitamtumainia Mungu,

maana nitamsifu tena Mungu,

aliye msaada wangu na Mungu wangu.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania