Zaburi 97

Zaburi 97

Mungu mtawala mkuu

1Mwenyezi-Mungu anatawala!

Furahi, ee dunia!

Furahini enyi visiwa vingi!

2Mawingu na giza nene vyamzunguka;

uadilifu na haki ni msingi wa utawala wake.

3Moto watangulia mbele yake,

na kuwateketeza maadui zake pande zote.

4Umeme wake wauangaza ulimwengu;

dunia yauona na kutetemeka.

5Milima yayeyuka kama nta mbele ya Mwenyezi-Mungu;

naam, mbele ya Bwana wa dunia yote.

6Mbingu zatangaza uadilifu wake;

na mataifa yote yauona utukufu wake.

7Wote wanaoabudu sanamu wanaaibishwa,

naam, wote wanaojisifia miungu duni;

miungu yote husujudu mbele zake.

8Watu wa Siyoni wanafurahi;

watu wa Yuda wanashangilia,

kwa sababu ya hukumu zako, ee Mungu.

9Wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu juu ya dunia yote;

wewe watukuka juu ya miungu yote.

10Mwenyezi-Mungu huwapenda wanaochukia uovu,

huyalinda maisha ya watu wake;

huwaokoa makuchani mwa waovu.

11Mwanga humwangazia mtu mwadilifu,

na furaha kwa watu wanyofu wa moyo.

12Furahini kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu;

mshukuruni kwa ajili ya jina lake takatifu.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania