Zaburi 118

Zaburi 118

Sala ya shukrani

1Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, kwa kuwa ni mwema,

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

2Watu wa Israeli na waseme:

“Fadhili zake zadumu milele.”

3Wazawa wa Aroni na waseme:

“Fadhili zake zadumu milele.”

4Wote wamchao Mwenyezi-Mungu na waseme:[#118:2-4 Vikundi vitatu vinatajwa kana kwamba vinajumuisha jamii yote. Kuhusu wazawa wa Aroni taz 115:10; na 99:6 maelezo.]

“Fadhili zake zadumu milele.”

5Katika taabu yangu nilimwomba Mwenyezi-Mungu,

naye akanisikia na kuniweka huru.

6Mwenyezi-Mungu yuko nami, siogopi kitu;

binadamu ataweza kunifanya nini?

7Mwenyezi-Mungu yuko nami, kunisaidia;

nami nitawaona maadui zangu wameshindwa.

8Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu,

kuliko kumtumainia mwanadamu.

9Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu,

kuliko kuwatumainia viongozi wa dunia.

10Mataifa yote yalinizingira,

lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu nikayaangamiza!

11Yalinizunguka kila upande,

lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu, nikayaangamiza!

12Yalinizunguka, mengi kama nyuki,

lakini yakateketea kama kichaka motoni;

kwa jina la Mwenyezi-Mungu niliyaangamiza!

13Nilishambuliwa mno karibu nishindwe,

lakini Mwenyezi-Mungu alinisaidia.

14Mwenyezi-Mungu ni nguvu yangu kuu;

yeye mwenyewe ndiye wokovu wangu.

15Sauti za furaha ya ushindi zasikika hemani mwao waadilifu:[#118:15 Yaani mahema ya vita au labda mahema ya muda ambamo watu walikusanyika wakati wa ibada. Wengine wanafikiri matumizi yake hapa ni ya jumla kwa maana ya makazi ya watu.]

“Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!

16Mkono wa nguvu wa Mwenyezi-Mungu umeleta ushindi!

Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!”

17Sitakufa, bali nitaishi,

na kusimulia matendo ya Mwenyezi-Mungu.

18Mwenyezi-Mungu ameniadhibu sana,

lakini hakuniacha nife.

19Nifungulie milango ya watu waadilifu,

niingie na kumshukuru Mwenyezi-Mungu!

20Huu ndio mlango wa Mwenyezi-Mungu,

watu waadilifu watapitia humo.

21Nakushukuru, ee Mungu kwa kunijibu;

kwa sababu wewe ni wokovu wangu.

22Jiwe walilokataa waashi,

limekuwa jiwe kuu la msingi.

23Hiyo ni kazi yake Mwenyezi-Mungu

nayo ni ya ajabu sana kwetu.

24Hii ndiyo siku aliyoifanya Mwenyezi-Mungu;

tushangilie na kufurahi.

25Tafadhali utuokoe, ee Mwenyezi-Mungu!

Tafadhali utufanikishe, ee Mwenyezi-Mungu!

26Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Mwenyezi-Mungu!

Twawabariki kutoka nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu

27Mwenyezi-Mungu ni Mungu;

yeye ametujalia mwanga wake

Shikeni matawi ya sherehe,

mkiandamana mpaka madhabahuni.

28Wewe ni Mungu wangu, nami ninakushukuru;

ninakutukuza, ee Mungu wangu.

29Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema,

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania