Zaburi 36

Zaburi 36

Uovu wa binadamu

1Dhambi huongea na mtu mwovu,[#36:1 Au, “Dhambi ni kauli ya mtu mwovu”.]

ndani kabisa moyoni mwake;

jambo la kumcha Mungu halimo kabisa kwake.

2Mwovu hujipendelea mwenyewe,

hufikiri uovu wake hautagunduliwa na kulaaniwa.

3Kila asemacho ni uovu na uongo;

ameacha kutumia hekima na kutenda mema.

4Alalapo huwaza kutenda maovu,

hujiweka katika njia isiyo njema,

wala haachani na uovu.

Wema wa Mungu

5Fadhili zako ee Mwenyezi-Mungu zaenea hata mbinguni;

uaminifu wako wafika mawinguni.

6Uadilifu wako ni kama milima mikubwa,

hukumu zako ni kama vilindi vya bahari.

Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, wawalinda wanadamu na wanyama

7Jinsi gani zilivyo bora fadhili zako!

Wanadamu hukimbilia kivulini mwa mabawa yako.

8Wawashibisha kwa utajiri wa nyumba yako;

wawanywesha kutoka mto wa wema wako.

9Wewe ndiwe asili ya uhai;

kwa mwanga wako twaona mwanga.

10Uendelee kuwafadhili wale wanaokutambua;

uzidi kuwa mwema kwa wanyofu wa moyo.

11Usikubali wenye majivuno wanivamie,

wala watu waovu wanikimbize.

12Kumbe watendao maovu wameanguka;

wameangushwa chini, hawawezi kuinuka.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania