Hosea 10

Hosea 10

1Israeli alikuwa mzabibu uliostawi sana,

alijizalia matunda mwenyewe.

Kadiri matunda yake yalivyoongezeka,

alijenga madhabahu zaidi;

kadiri nchi yake ilivyostawi,

alipamba mawe yake ya ibada.

2Moyo wao ni mdanganyifu,

nao sasa lazima wachukue hatia yao.

Bwana atabomoa madhabahu zao

na kuharibu mawe yao ya ibada.

3Kisha watasema, “Hatuna mfalme

kwa sababu hatukumheshimu Bwana .

Lakini hata kama tungekuwa na mfalme,

angeweza kutufanyia nini?”

4Wanaweka ahadi nyingi,

huapa viapo vya uongo

wanapofanya mapatano;

kwa hiyo mashtaka huchipuka

kama magugu ya sumu

katika shamba lililolimwa.

5Watu wanaoishi Samaria huogopa

kwa ajili ya sanamu ya ndama ya Beth-Aveni.

Watu wake wataiombolezea,

vivyo hivyo kuhani wake wa kuabudu sanamu,

wale waliokuwa wamefurahia fahari yake,

kwa sababu itaondolewa kutoka kwao

kwenda uhamishoni.

6Itachukuliwa kwenda Ashuru

kama ushuru kwa mfalme mkuu.

Efraimu atafedheheshwa;

Israeli ataaibika kwa ajili ya sanamu zake za mti.

7Samaria na mfalme wake wataelea

kama kijiti juu ya maji.

8Mahali pa juu pa uovu pataharibiwa:[#10:8 yaani Aveni kwa Kiebrania, kumaanisha Beth-Aveni]

ndiyo dhambi ya Israeli.

Miiba na mibaruti itaota

na kufunika madhabahu zao.

Kisha wataiambia milima, “Tufunikeni!”

na vilima, “Tuangukieni!”

9“Tangu siku za Gibea, umetenda dhambi, ee Israeli,

huko ndiko ulibaki.

Je, vita havikuwapata

watenda maovu huko Gibea?

10Wakati nitakapopenda, nitawaadhibu;

mataifa yatakusanywa dhidi yao

ili kuwaweka katika vifungo

kwa ajili ya dhambi zao mbili.

11Efraimu ni ndama jike aliyefundishwa

ambaye hupenda kupura;

hivyo nitamfunga nira

juu ya shingo yake nzuri.

Nitamwendesha Efraimu,

Yuda lazima alime,

naye Yakobo lazima avunjavunje

mabonge ya udongo.

12Jipandieni wenyewe haki,

vuneni matunda ya upendo usio na kikomo,

vunjeni ardhi yenu isiyolimwa;

kwa kuwa ni wakati wa kumtafuta Bwana ,

hadi atakapokuja

na kuwanyeshea juu yenu haki.

13Lakini mmepanda uovu,

mkavuna ubaya,

mmekula tunda la udanganyifu.

Kwa sababu mmetegemea nguvu zenu wenyewe

na wingi wa mashujaa wenu,

14mngurumo wa vita utainuka dhidi ya watu wako,

na ngome zako zote zitaharibiwa:

kama Shalmani alivyoharibu Beth-Arbeli katika siku ile ya vita,

wakati mama pamoja na watoto wao

walipotupwa kwa nguvu ardhini.

15Ndivyo itakavyotokea kwako, ee Betheli,

kwa sababu uovu wako ni mkuu.

Siku ile itakapopambazuka,

mfalme wa Israeli ataharibiwa kabisa.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.