Isaya 2

Isaya 2

Mlima wa Bwana

(Mik 4:1‑3)

1Hili ndilo aliloliona Isaya mwana wa Amozi kuhusu Yuda na Yerusalemu:

2Katika siku za mwisho

mlima wa Hekalu la Bwana utaimarishwa

kama mlima mkuu miongoni mwa milima yote,

utainuliwa juu ya vilima,

na mataifa yote yatamiminika huko.

3Mataifa mengi yatakuja na kusema,

“Njooni, twendeni kwenye mlima wa Bwana ,

kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo.

Atatufundisha njia zake,

ili tuweze kuenenda katika mapito yake.”

Sheria itatoka Sayuni,

neno la Bwana litatoka Yerusalemu.

4Atahukumu kati ya mataifa

na ataamua migogoro ya mataifa mengi.

Watafua panga zao ziwe majembe,

na mikuki yao kuwa miundu ya kukata matawi.

Taifa halitainua upanga dhidi ya taifa jingine,

wala hawatajifunza vita tena.

5Njooni, enyi nyumba ya Yakobo,

tutembeeni katika nuru ya Bwana .

Siku ya Bwana

6Bwana umewatelekeza watu wako,

nyumba ya Yakobo.

Wamejaa ushirikina unaotoka Mashariki,

wanapiga ramli kama Wafilisti

na wanashikana mikono na wapagani.

7Nchi yao imejaa fedha na dhahabu,

hakuna mwisho wa hazina zao.

Nchi yao imejaa farasi,

hakuna mwisho wa magari yao ya vita.

8Nchi yao imejaa sanamu;

wanasujudia kazi za mikono yao,

vitu vile vidole vyao vimevitengeneza.

9Kwa hiyo mwanadamu atashushwa

na binadamu atanyenyekezwa:

usiwasamehe.

10Ingieni kwenye miamba,

jificheni ardhini

kutokana na utisho wa Bwana

na utukufu wa enzi yake!

11Macho ya mtu mwenye majivuno yatanyenyekezwa

na kiburi cha wanadamu kitashushwa,

Bwana peke yake ndiye atakayetukuzwa siku hiyo.

12Bwana wa majeshi anayo siku aliyoiweka akiba

kwa wote wenye kujivuna na wenye kiburi,

kwa wote wanaojikweza

(nao watanyenyekezwa),

13kwa mierezi yote ya Lebanoni iliyo mirefu sana,

na mialoni yote ya Bashani,

14kwa milima yote mirefu

na vilima vyote vilivyoinuka,

15kwa kila mnara ulio mrefu sana

na kila ukuta wenye ngome,

16kwa kila meli ya biashara,[#2:16 au ya Tarshishi (taz. 1Fal 10:22; 22:48; 2Nya 9:21; 20:36; Isa 60:9).]

na kila mashua ya kifahari.

17Majivuno ya mwanadamu yatashushwa,

na kiburi cha wanadamu kitanyenyekezwa,

Bwana peke yake ndiye atatukuzwa siku hiyo,

18nazo sanamu zitatoweka kabisa.

19Watu watakimbilia kwenye mapango ndani ya miamba,

na kwenye mahandaki ardhini

kutokana na utisho wa Bwana

na utukufu wa enzi yake,

ainukapo kuitikisa dunia.

20Siku ile, watu watawatupia

panya na popo

sanamu zao za fedha na za dhahabu,

walizozitengeneza ili waziabudu.

21Watakimbilia kwenye mapango miambani

na kwenye nyufa za miamba

kutokana na utisho wa Bwana

na utukufu wa enzi yake,

ainukapo kuitikisa dunia.

22Acheni kumtumainia mwanadamu,

ambaye hana kitu ila pumzi katika pua zake.

Yeye ana thamani gani?

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.