Zaburi 56

Zaburi 56

Zaburi 56

Kumtumaini Mungu

1Ee Mungu unihurumie, maana watu wananifuatia vikali;

mchana kutwa wanazidisha mashambulizi yao.

2Wasingiziaji wangu wananifuatia mchana kutwa,

wengi wananishambulia kwa kiburi chao.

3Wakati ninaogopa,

nitakutumaini wewe.

4Katika Mungu, ambaye neno lake ninalisifu,

katika Mungu ninatumaini, sitaogopa.

Mwanadamu mwenye kufa

atanitenda nini?

5Mchana kutwa wanayageuza maneno yangu,

siku zote wanapanga njama za kunidhuru.

6Wananifanyia hila, wanajificha,

wanatazama hatua zangu,

wakiwa na shauku ya kuutoa uhai wangu.

7Wasiepuke kwa vyovyote,

Ee Mungu, katika hasira yako yaangushe mataifa.

8Andika maombolezo yangu;

andika machozi yangu katika kitabu chako:

je, haya hayapo katika kumbukumbu zako?

9Ndipo adui zangu watarudi nyuma

ninapoita msaada.

Kwa hili nitajua kwamba Mungu

yuko upande wangu.

10Katika Mungu, ambaye neno lake ninalisifu,

katika Bwana , ambaye neno lake ninalisifu,

11katika Mungu ninatumaini, sitaogopa.

Mwanadamu anaweza kunitenda nini?

12Ee Mungu, nina nadhiri kwako,

nitakutolea wewe sadaka zangu za shukrani.

13Kwa kuwa umeniokoa toka kwenye mauti

na miguu yangu kwenye kujikwaa,

ili niweze kuenenda mbele za Mungu

katika nuru ya uzima.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.