Yona 4

Yona anaonywa na Bwana.

1Hivi vikamkasirisha Yona sana na kumchafua moyo wake,[#2 Mose 34:6.]

2akamwomba Bwana kwamba: E Bwana, haya siyo, niliyoyasema nilipokuwa katika nchi ya kwetu? Kwa hiyo naliondoka kukimbilia Tarsisi, kwani nalijua, ya kuwa wewe ndiwe Mungu mwenye utu na huruma, tena u mwenye uvumilivu na upole mwingi, hugeuza moyo, usifanye mabaya.

3Sasa, Bwana, jitwalie roho yangu, initoke! Kwani kufa kwangu ni kwema kuliko kuishi.[#1 Fal. 19:4.]

4Bwana akamjibu: Je? Ni vema ukichafuka hivyo?

5Kisha Yona akatoka mle mjini, akakaa nje ya mji upande wa maawioni kwa jua, akajijengea kibanda kidogo, akakaa chini yake kivulini, mpaka aone, mambo ya mji yatakavyokuwa.[#Yona 4:9.]

6Bwana Mungu akaagiza mbonobono, akauotesha, uwe juu ya mahali pake Yona, umpatie kivuli cha kichwa chake, uondoe hivyo ubaya moyoni mwake. Yona akaufurahia sana huo mbonobono.

7Lakini kulipopambazuka siku ya kesho kutwa, Mungu akaagiza kidudu, kikautoboa huo mbonobono, ukanyauka.

8Ikawa, jua lilipopanda juu, Mungu akaagiza upepo wenye joto utokao upande wa maawioni kwa jua; basi, jua lilipompiga Yona kichwani, akazimia, akajitakia kufa akisema: Kufa kwangu ni kwema kuliko kuishi.

9Mungu akamwambia Yona: Je? Ni vema, ukichafuka hivyo kwa ajili ya mbonobono? Akajibu: Ndio, ni vema, nikikasirika, mpaka nife.[#Yona 4:4.]

10Bwana akamwambia: Wewe unauonea mbonobono huu uchungu, tena hukuusumbukia, wala hukuukuza; uliota na usiku, tena umekufa na usiku mwingine.

11Nami nisiuonee uchungu mji huu mkubwa wa Niniwe, kwa kuwa humu wamo watu kupita 120000 wasiojua kupambanua yaliyoko kuumeni nayo yaliyoko kushotoni? Tena wamo nyama wengi.[#Yona 3:3.]

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania