The chat will start when you send the first message.
1Basi hata agano la kwanza lilikuwa na kawaida za ibada, na patakatifu pake, pa kidunia.
2Maana hema ilitengenezwa, ile ya kwanza, mlimokuwa na kinara cha taa, na meza, na mikate mitakatifu; ndipo palipoitwa, Patakatifu.[#Kut 26:1-30; 25:23-40]
3Na nyuma ya pazia la pili, ile hema iitwayo Patakatifu pa patakatifu,[#Kut 26:31-33]
4yenye chetezo cha dhahabu, na sanduku la Agano lililofunikwa kwa dhahabu pande zote, mlimokuwa na kopo la dhahabu lenye ile mana, na ile fimbo ya Haruni iliyochipuka, na vile vibao vya agano;[#Kut 16:33; 25:10-16,21; 30:1-6; Hes 17:8-10; Kum 10:3-5]
5na juu yake makerubi ya utukufu, yakikitia kivuli kiti cha rehema; basi hatuna nafasi sasa ya kueleza habari za vitu hivi kimoja kimoja.[#Kut 25:18-22; 26:34]
6Basi, vitu hivi vikiisha kutengenezwa hivyo, makuhani huingia katika hema hiyo ya kwanza daima, wakiyatimiza mambo ya ibada.[#Hes 18:2-6]
7Lakini katika hema hiyo ya pili kuhani mkuu huingia peke yake, mara moja kila mwaka; wala si pasipo damu, atoayo kwa ajili ya nafsi yake na kwa dhambi walizozitenda hao watu bila kujua.[#Law 16:2-34; Kut 30:10]
8Roho Mtakatifu akionesha neno hili, ya kwamba njia ya kupaingia patakatifu ilikuwa haijadhihirishwa bado, hapo hema ya kwanza ilipokuwa ingali ikisimama;[#Ebr 10:19]
9ambayo ndiyo mfano wa wakati huu ulioko sasa; wakati huo sadaka na dhabihu zinatolewa, zisizoweza kwa jinsi ya dhambi kumkamilisha mtu aabuduye,[#Ebr 10:1,2]
10kwa kuwa ni sheria za jinsi ya mwili tu, vyakula na vinywaji na kunawa kwingine kwingine, zilizoamriwa hata wakati wa matengenezo mapya.[#Law 11:2; 15:18; Hes 19:13]
11Lakini Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa mambo mema yatakayokuwapo, kwa hema iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika kwa mikono, maana yake, isiyo ya ulimwengu huu,[#Ebr 6:20; 10:1]
12wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele.
13Kwa maana, ikiwa damu ya mbuzi na mafahali na majivu ya ndama ya ng'ombe waliyonyunyiziwa wenye uchafu hutakasa hata kuusafisha mwili;[#Law 16:3,15-16; Hes 19:9,17-19]
14basi si zaidi damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na dosari, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu, mpate kumwabudu Mungu aliye hai?[#1 Pet 1:18,19; 1 Yoh 1:7; Ufu 1:5; 1 Kor 15:45; Ebr 6:1]
15Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele.[#Ebr 12:24; 1 Tim 2:5]
16Maana agano la urithi lilipo, lazima iwepo mauti yake aliyelifanya.
17Kwa maana agano la urithi lina nguvu palipotukia kufa kwa mtu; kwa kuwa halina nguvu kabisa, akiwa yu hai yeye aliyelifanya.
18Kwa hiyo hata lile la kwanza halikuanzwa pasipo damu.
19Maana kila amri ilipokwisha kunenwa na Musa kwa hao watu wote, kama ilivyoamuru sheria, aliitwaa damu ya ndama na ya mbuzi, pamoja na maji na sufu nyekundu na hisopo, akakinyunyizia kitabu chenyewe, na watu wote,[#Kut 24:6-8; Law 14:4; Hes 19:6]
20akisema, Hii ni damu ya agano mliloamriwa na Mungu.[#Mt 26:28]
21Na ile hema nayo na vyombo vyote vya ibada alivinyunyizia damu vivyo hivyo.[#Law 8:15,19]
22Na katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo.[#Law 17:11; Efe 1:7]
23Basi ilikuwa sharti nakala za mambo yaliyo mbinguni zisafishwe kwa hizo, lakini mambo ya mbinguni yenyewe yasafishwe kwa dhabihu zilizo bora kuliko hizo.[#Ebr 8:5]
24Kwa sababu Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu;[#Ebr 11:12; 1 Yoh 2:1]
25wala si kwamba ajitoe mara nyingi, kama vile kuhani mkuu aingiavyo katika patakatifu kila mwaka kwa damu isiyo yake;
26kama ni hivyo, ingalimpasa kuteswa mara nyingi tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu; lakini sasa, mara moja tu, katika utimilifu wa nyakati, amefunuliwa, azitangue dhambi kwa dhabihu ya nafsi yake.[#1 Kor 10:11; Gal 4:4]
27Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu;[#Mwa 3:19]
28kadhalika Kristo naye, akiisha kutolewa sadaka mara moja azichukue dhambi za watu wengi; atatokea mara ya pili, pasipo dhambi, kwa hao wamtazamiao kwa wokovu.[#Isa 53:12; Flp 3:20; Ebr 10:10; 12:14; 2 Tim 4:8; 1 Pet 2:24]