Isaya 53

Isaya 53

1Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta?[#1 Kor 1:18; Yn 12:38; Rum 10:16]

Na mkono wa BWANA amefunuliwa nani?

2Maana alikuwa mbele zake kama mche mwororo,[#Mk 9:12]

Na kama mzizi katika nchi kavu;

Yeye hana umbo wala uzuri;

Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.

3Alidharauliwa na kukataliwa na watu;[#Zab 22:6; Ebr 4:15; Yn 1:10]

Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko;

Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao,

Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.

4Hakika ameyachukua masikitiko yetu,[#Mt 8:17; 26:66; 1 Pet 2:24]

Amejitwika huzuni zetu;

Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa,

Amepigwa na Mungu, na kuteswa.

5Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu,[#1 Pet 2:24]

Alichubuliwa kwa maovu yetu;

Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake,

Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.

6Sisi sote kama kondoo tumepotea;[#1 Pet 2:25]

Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe;

Na BWANA ameweka juu yake

Maovu yetu sisi sote.

7Alionewa, lakini alinyenyekea,[#Mdo 8:32; 1 Pet 1:19; Ufu 5:6]

Wala hakufunua kinywa chake;

Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni,

Na kama vile kondoo anyamazavyo

Mbele yao wakatao manyoya yake;

Naam, hakufunua kinywa chake.

8Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa;[#Dan 9:26]

Na maisha yake ni nani angeyajali?

Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai;

Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu.

9Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya;[#Mt 27:57; 1 Pet 2:22]

Na pamoja na matajiri katika kufa kwake;

Ingawa hakutenda jeuri,

Wala hapakuwa na hila kinywani mwake.

10Lakini BWANA aliridhika kumchubua;[#2 Kor 5:21; Gal 3:13; Rum 6:9; Efe 1:5]

Amemhuzunisha;

Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi,

Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi,

Na mapenzi ya BWANA yatafanikiwa mkononi mwake;

11Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika.[#Yn 17:3; 1 Yoh 2:1; Rum 5:18]

Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki

Atawafanya wengi kuwa wenye haki;

Naye atayachukua maovu yao.

12Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu,[#Flp 2:9; Kol 2:15; Mk 15:28; Lk 22:37; 23:34]

Naye atagawana nyara pamoja nao walio hodari;

Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa,

Akahesabiwa pamoja na hao wakosao.

Walakini alichukua dhambi za watu wengi,

Na kuwaombea wakosaji.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya