Zaburi 6

Zaburi 6

Sala wakati wa taabu

1Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako;[#6:1 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa hapa ni zito zaidi; linajumuisha pia maana ya “kupatiliza”.]

usiniadhibu kwa ghadhabu yako.

2Unihurumie, ee Mwenyezi-Mungu, nimeishiwa nguvu;

uniponye, ee Mwenyezi-Mungu, nataabika mpaka mifupani.

3Ninahangaika sana rohoni mwangu.

Ee Mwenyezi-Mungu, utakawia mpaka lini?

4Unigeukie, ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe;

unisalimishe kwa sababu ya fadhili zako.

5Huko kwa wafu hakuna anayekukumbuka;[#6:5 Yaani kuzimu. Ilifikiriwa kwamba kifo kilimweka mtu mbali na Mungu hata asiweze tena kumwabudu na kumsifu (taz Yobu 10:21-22; Isa 38:18). “Hakuna anayekukumbuka”, yaani kumsifu na kumwomba. Kumkumbuka Mwenyezi-Mungu ni kusimulia mambo aliyowatendea watu wake.]

huko kuzimu ni nani awezaye kukusifu?

6Niko hoi kwa kilio cha uchungu;

kila usiku nalowesha kitanda changu kwa machozi;

kwa kulia kwangu naulowesha mto wangu.

7Macho yangu yamechoka kwa huzuni;

yamefifia kwa kutaabishwa na adui.

8Ondokeni kwangu enyi nyote watenda maovu!

Maana Mwenyezi-Mungu amesikia kilio changu.

9Mwenyezi-Mungu amesikia ombi langu;

Mwenyezi-Mungu amekubali sala yangu.

10Maadui zangu wote wataaibika na kufadhaika;[#6:10 Kitenzi “wataaibika” ni tukio linalofuata adhabu ya Mungu na kushindwa kwa hao maadui.]

watarudi nyuma na kuaibishwa ghafla.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania