Mithali 7

Mithali 7

Onyo dhidi ya mwanamke mzinzi

1Mwanangu, shika maneno yangu

na kuzihifadhi amri zangu ndani yako.

2Shika amri zangu nawe utaishi;

linda mafundisho yangu kama mboni ya jicho lako.

3Yafunge katika vidole vyako;

yaandike katika kibao cha moyo wako.

4Mwambie hekima, “Wewe ni dada yangu,”

uite ufahamu jamaa yako;

5watakuepusha na mwanamke mzinzi,

kutokana na mwanamke mpotovu

na maneno yake ya kubembeleza.

6Kwenye dirisha la nyumba yangu

nilitazama nje kupitia upenyo

kwenye mwimo wa dirisha.

7Niliona miongoni mwa wajinga,

nikagundua miongoni mwa wanaume vijana,

kijana asiye na akili.

8Alikuwa akishuka njiani karibu na pembe ya kwake,

akielekea kwenye nyumba ya huyo mwanamke

9wakati wa machweo, jua likipungua nuru yake,

giza la usiku lilipokuwa likiingia.

10Ndipo huyo mwanamke akatoka kumlaki,

hali amevaa kama kahaba akiwa na nia ya hila.

11(Ni mwanamke mwenye makelele na mkaidi,

miguu yake haitulii nyumbani;

12mara kwenye barabara za mji,

mara kwenye viwanja vikubwa,

kwenye kila pembe huvizia.)

13Huyo mwanamke alimkumbatia kijana na kumbusu,

na kwa uso usio na haya akamwambia:

14“Nina sadaka za amani nyumbani;

leo nimetimiza nadhiri zangu.

15Kwa hiyo nimetoka nje kukulaki;

nimekutafuta na nimekupata!

16Nimetandika kitanda changu

kwa kitani za rangi kutoka Misri.

17Nimetia manukato kitanda changu

kwa manemane, udi na mdalasini.

18Njoo, tuzame katika mapenzi hadi asubuhi;

tujifurahishe wenyewe kwa mapenzi!

19Mume wangu hayupo nyumbani;

ameenda safari ya mbali.

20Amechukua mkoba uliojazwa fedha

na hatakuwa nyumbani karibuni.”

21Kwa maneno laini yule mwanamke akampotosha;

alimshawishi kwa maneno yake laini.

22Mara huyo kijana alimfuata yule mwanamke

kama fahali aendaye machinjoni,

kama kulungu aingiaye kwenye kitanzi,

23hadi mshale umchome ini lake,

kama ndege anayenaswa kwenye mtego,

bila kujua itamgharimu maisha yake.

24Sasa basi wanangu, nisikilizeni;

sikilizeni kwa makini nisemalo.

25Usiruhusu moyo wako ugeukie njia za huyo mwanamke,

wala usitangetange katika mapito yake.

26Aliowaangusha ni wengi;

aliowachinja ni kundi kubwa.

27Nyumba yake ni njia kuu iendayo kaburini,[#7:27 Kaburini hapa maana yake ni Kuzimu ; kwa Kiebrania ni Sheol.]

ielekeayo chini kwenye vyumba vya mauti.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.