Zaburi 144

Zaburi 144

Zaburi 144

Mfalme amshukuru Mwenyezi Mungu kwa ushindi

1Ahimidiwe Mwenyezi Mungu Mwamba wangu,

aifundishaye mikono yangu vita,

na vidole vyangu kupigana.

2Yeye ni Mungu wangu wa upendo na ulinzi wangu,

ngome yangu na mwokozi wangu,

ngao yangu, ninayemkimbilia,

ambaye huwatiisha mataifa chini yangu.

3Ee Mwenyezi Mungu, mwanadamu ni nini hata umjali,

Binadamu ni nini hata umfikirie?

4Mwanadamu ni kama pumzi,

siku zake ni kama kivuli kinachopita.

5Ee Mwenyezi Mungu, pasua mbingu zako, ushuke,

gusa milima ili itoe moshi.

6Peleka umeme uwatawanye adui,

lenga mishale yako uwashinde.

7Nyoosha mkono wako kutoka juu,

nikomboe na kuniokoa

kutoka maji makuu,

kutoka mikononi mwa wageni

8ambao vinywa vyao vimejaa uongo,

na mikono yao ya kuume ni midanganyifu.

9Ee Mungu, nitakuimbia wimbo mpya,

kwa zeze yenye nyuzi kumi nitakuimbia,

10kwa Yule awapaye wafalme ushindi,

ambaye humwokoa Daudi, mtumishi wake,

kutokana na upanga hatari.

11Nikomboe na uniokoe

kutoka mikononi mwa wageni

ambao vinywa vyao vimejaa uongo,

na mikono yao ya kuume ni midanganyifu.

12Kisha wana wetu wakati wa ujana wao

watakuwa kama mimea iliyotunzwa vizuri,

binti zetu watakuwa kama nguzo zilizoviringwa

kurembesha jumba la kifalme.

13Ghala zetu zitajazwa

aina zote za mahitaji.

Kondoo wetu watazaa kwa maelfu,

kwa makumi ya maelfu katika mashamba yetu;

14maksai wetu watakokota

mizigo mizito.

Hakutakuwa na kubomoka kuta,

hakuna kuchukuliwa mateka,

wala kilio cha taabu

katika barabara zetu.

15Heri watu ambao hili ni kweli;

heri wale ambao Mwenyezi Mungu ni Mungu wao.

Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™ Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Scriptures™ Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.