Zaburi 17

Zaburi 17

Zaburi 17

Sala ya mtu asiye na hatia

1Sikia, Ee Bwana , kusihi kwangu kwa haki,

sikiliza kilio changu.

Tega sikio kwa ombi langu,

halitoki katika midomo ya udanganyifu.

2Hukumu yangu na itoke kwako,

macho yako na yaone yale yaliyo haki.

3Ingawa unauchunguza moyo wangu na kunikagua usiku,

ingawa umenijaribu, hutaona chochote.

Nimeamua kwamba kinywa changu

hakitatenda dhambi.

4Kuhusu matendo ya wanadamu:

kwa neno la midomo yako,

nimejiepusha na njia za wenye jeuri.

5Hatua zangu zimeshikamana na njia zako;

nyayo zangu hazikuteleza.

6Ee Mungu, ninakuita, kwa kuwa utanijibu,

nitegee sikio lako na usikie ombi langu.

7Uoneshe ajabu ya upendo wako mkuu,

wewe unayeokoa kwa mkono wako wa kuume

wale wanaokukimbilia kutokana na adui zao.

8Nilinde kama mboni ya jicho lako,

unifiche chini ya kivuli cha mabawa yako

9kutokana na waovu wanaonishambulia,

kutokana na adui wauaji wanaonizunguka.

10Huifunga mioyo yao iliyo migumu,

vinywa vyao hunena kwa majivuno.

11Wamenifuatia nyayo zangu, sasa wamenizingira,

wakiwa macho, waniangushe chini.

12Wamefanana na simba mwenye njaa anayewinda,

kama simba mkubwa anayenyemelea mafichoni.

13Inuka, Ee Bwana , pambana nao, uwaangushe,

niokoe kwa upanga wako kutoka kwa waovu.

14Ee Bwana , mkono wako uniokoe na watu kama hawa,

kutokana na watu wa ulimwengu huu

ambao fungu lao liko katika maisha haya.

Na wapate adhabu ya kuwatosha.

Watoto wao na wapate zaidi ya hayo,

hukumu na iendelee kwa watoto wa watoto wao.

15Bali mimi nitauona uso wako katika haki;

niamkapo, nitaridhika kwa kuona sura yako.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.