Zaburi 30

Zaburi 30

Zaburi 30

Maombi ya shukrani

1Nitakutukuza wewe, Ee Bwana ,

kwa kuwa umeniinua kutoka vilindi,

na hukuacha adui zangu

washangilie juu yangu.

2Ee Bwana Mungu wangu, nilikuita unisaidie

na wewe umeniponya.

3Ee Bwana , umenitoa Kuzimu,[#30:3 Kuzimu kwa Kiebrania ni Sheol , yaani Shimo lisilo na mwisho.]

umeniokoa nisishuke kwenye shimo la mauti.

4Mwimbieni Bwana , enyi watakatifu wake;

lisifuni jina lake takatifu.

5Kwa maana hasira yake ni ya muda mfupi,

bali upendo wake hudumu siku zote.

Inawezekana kilio kiwepo usiku kucha,

lakini furaha huja asubuhi.

6Nilipofanikiwa nilisema,

“Sitatikiswa kamwe.”

7Ee Bwana , uliponijalia,

uliuimarisha mlima wangu,

lakini ulipouficha uso wako

nilifadhaika.

8Kwako wewe, Ee Bwana , niliita,

niliomba rehema kwa Bwana:

9“Kuna faida gani katika kuangamia kwangu,

katika kushuka kwangu shimoni?

Je, mavumbi yatakusifu?

Je, yatatangaza uaminifu wako?

10Ee Bwana , unisikie na kunihurumia;

Ee Bwana , uwe msaada wangu.”

11Uligeuza maombolezo yangu kuwa kucheza,

ulinivua gunia ukanivika shangwe,

12ili moyo wangu uweze kukusifu na usikae kimya.

Ee Bwana Mungu wangu, nitakushukuru milele.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.