Mhubiri 10

Mhubiri 10

Maoni mengine

1Nzi waliokufa hufanya manukato ya mwuza marashi kutoa uvundo;

Kadhalika upumbavu haba ni mzito kuliko hekima na heshima.

2Moyo wake mwenye hekima upo upande wa kulia;[#Mt 6:33; Kol 3:1]

Bali moyo wake mpumbavu upo mkono wa kushoto.

3Naam, huyo mpumbavu tena, aendapo njiani, hupungukiwa na fahamu zake; hata humwambia kila mtu ya kuwa yeye ni mpumbavu.[#Mit 13:16]

4Roho yake mtawala ikiinuka kinyume chako,[#Mhu 8:3; 1 Sam 25:24; Mit 25:15]

Usiondoke mara mahali pako ulipo;

Kwa maana roho ya upole hutuliza machukizo yaliyo makubwa.

5Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye;

6ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi hukaa mahali pa chini.

7Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.[#Mit 19:10]

8Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake;[#Zab 7:15; Mit 26:27]

Na yeye abomoaye boma, nyoka atamwuma.

9Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo;

Naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo.

10Iwapo chuma hakipati, wala mtu hakinoi;

Ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi. Lakini yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa.

11Nyoka akiuma kabla hajachezeshwa,[#Yer 8:17]

Basi hakuna faida ya mchezeshaji.

12Maneno ya kinywa chake mwenye hekima yana neema;

Bali midomo ya mpumbavu itammeza nafsi yake.

13Mwanzo wa maneno ya kinywa chake ni upuuzi; na mwisho wa usemi wake ni wazimu wenye hatari.

14Tena, upumbavu huongeza maneno; lakini mwanadamu hajui yatakayokuwako; nayo yatakayokuwa baada yake, ni nani awezaye kumweleza?[#Yak 4:14]

15Kazi yao wapumbavu huwachosha kila mmoja,

Maana hajui hata njia ya kuuendea mji.

16Ole wako, nchi, iwapo mfalme wako ni kijana,[#Isa 3:4]

Na wakuu wako hula asubuhi!

17Heri kwako, nchi, mfalme wako akiwa mtoto wa watu,[#Mit 31:4]

Na wakuu wako hula wakati ufaao, Ili makusudi wapate nguvu, wala si kwa ajili ya ulevi.

18Kwa sababu ya uvivu paa hunepa;

Na kwa ulegevu wa mikono nyumba huvuja.

19Karamu hufanywa kwa ajili ya kicheko,

Na divai huyafurahisha maisha; Na fedha huleta jawabu la mambo yote.

20Usimlaani mfalme, la, hata katika wazo lako;[#Kut 22:28]

Wala usiwalaani wakwasi chumbani mwako;

Kwa kuwa ndege wa anga ataichukua sauti,

Na mwenye mabawa ataitoa habari.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya