Zaburi 137

Zaburi 137

Ombolezo ugenini

1Kando ya mito ya Babuloni, tulikaa,

tukawa tunalia tulipokumbuka Siyoni.

2Katika miti ya nchi ile,

tulitundika zeze zetu.

3Waliotuteka walitutaka tuwaimbie;

watesi wetu walitutaka tuwafurahishe:

“Tuimbieni mojawapo ya nyimbo za Siyoni!”

4Twawezaje kuimba wimbo wa Mwenyezi-Mungu

katika nchi ya kigeni?

5Ee Yerusalemu, kama nikikusahau,

mkono wangu wa kulia na ukauke!

6Ulimi wangu na uwe mzito,

kama nisipokukumbuka wewe, ee Yerusalemu;

naam, nisipokuthamini kuliko furaha yangu kubwa!

7Ee Mwenyezi-Mungu, usisahau waliyotenda Waedomu,

siku ile Yerusalemu ilipotekwa;

kumbuka waliyosema:

“Bomoeni mji wa Yerusalemu!

Ngoeni hata na misingi yake!”

8Ee Babuloni, utaangamizwa![#Taz Ufu 18:6]

Heri yule atakayekulipiza mabaya uliyotutenda!

9Heri yule atakayewatwaa watoto wako

na kuwapondaponda mwambani!

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania