The chat will start when you send the first message.
1Basi, wewe mwanangu, uwe na nguvu katika neema tunayopata katika kuungana na Kristo Yesu.
2Chukua yale mafundisho uliyonisikia nikitangaza mbele ya mashahidi wengi, uyakabidhi kwa watu wanaoaminika, ambao wataweza kuwafundisha wengine pia.[#2:2 Tafsiri nyingine yamkini “kwa njia ya mashahidi” au, “kwa msaada wa mashahidi”. Kabla ya hapo, katika 1Tim 6:20, Paulo alikuwa amesema maneno kama hayo ya kumtia moyo Timotheo aendelee na bidii yake nyakati zote. Wengine wanafikiri yahusu wakati Timotheo alipowekwa wakfu.]
3Shiriki katika mateso kama askari mwaminifu wa Kristo Yesu.[#2:3 2Tim 1:8,12; 3:13; rejea Rom 8:17; Fil 1:29; 3:10. Katika baadhi ya aya hizi zilizotajwa, nyingine zinahusu kushiriki mateso ya Kristo, na nyingine mateso kwa jumla kutokana na kazi ya kuhubiri Injili.; #2:3-6 Katika aya hizi tuna picha tatu zinazomweleza mtume na kazi yake: picha ya askari, picha ya mwanariadha na picha ya mkulima; mifano hiyo mitatu imechagua katika kila moja sifa zinazotakiwa ikiwa ni pamoja na kujinyima mambo fulanifulani na kujipa nidhamu ili kupata mafanikio. Paulo anaunganisha picha hizo pia katika 1Kor 9:6-7,24-27.]
4Mwanajeshi vitani hujiepusha na shughuli za maisha ya kawaida, ili aweze kumpendeza mkuu wa jeshi.[#2:3-4 Fil 2:25; File 2. Kuhusu picha ya utumishi katika jeshi, taz 1Tim 1:18-20 maelezo.]
5Mwanariadha yeyote hawezi kushinda na kupata zawadi ya ushindi kama asipozitii sheria za michezo.
6Mkulima ambaye amefanya kazi ngumu anastahili kupata sehemu ya kwanza ya mavuno.
7Fikiria hayo ninayosema, kwani Bwana atakuwezesha uelewe kila kitu.
8Mkumbuke Yesu Kristo aliyefufuliwa kutoka kwa wafu, aliyekuwa wa ukoo wa Daudi, kama isemavyo Habari Njema ninayoihubiri,[#2:8 Maneno hayo yanaweza kufikiriwa kuwa miongoni mwa maneno ya msingi ya imani ya Wakristo wa kwanza, au muhtasari wa Injili. Rom 1:3-4 ni kipande kimojawapo kinachofanana na hiki. Tazama 2Tim 1:9. “wa ukoo wa Daudi”: Mojawapo ya vipengele vya kuonesha kwamba Yesu alikuwa Masiha au Kristo.]
9na ambayo kwa sababu yake mimi nateseka na nimefungwa minyororo kama mhalifu. Lakini neno la Mungu haliwezi kufungwa minyororo.[#2:9 Paulo amekuwa akiendelea na huduma yake ya kuhubiri neno la Mungu hata akiwa amefungwa gerezani (taz 2Tim 4:17; rejea Fil 1:12-14).]
10Kwa hiyo navumilia kila kitu kwa ajili ya wateule wa Mungu, ili wao pia wapate ukombozi upatikanao kwa njia ya Yesu Kristo, na ambao huleta utukufu wa milele.
11Usemi huu ni wa kweli:[#2:11 Maneno haya yanatumiwa mara kwa mara katika hizi Barua za kichungaji. Taz 1Tim 1:15 maelezo.]
“Ikiwa tulikufa pamoja naye,
tutaishi pia pamoja naye.
12Tukiendelea kuvumilia,
tutatawala pia pamoja naye.
Tukimkana,
naye pia atatukana.
13Tukikosa kuwa waaminifu,
yeye hubaki mwaminifu daima,
maana yeye hawezi kujikana mwenyewe.”
14Basi, wakumbushe watu wako mambo haya na kuwaonya mbele ya Mungu waache ubishi juu ya maneno. Ubishi huo haufai, ila huleta tu uharibifu mkuu kwa wale wanaousikia.
15Jitahidi kupata kibali kamili mbele ya Mungu kama mfanyakazi ambaye haoni haya juu ya kazi yake na ambaye hufundisha sawa ule ujumbe wa kweli.[#2:15 Pamoja na aya ya 14 na 16 ni dhahiri hapa kwamba yahusu kutangaza Injili ilivyo sawasawa na kuitangaza kwa unyofu, yaani kusema tu ule ukweli wake bila kuupinda (18).]
16Jiepushe na majadiliano yasiyofaa na ya kipumbavu; kwani hayo huzidi kuwatenga watu mbali na Mungu.
17Mafundisho ya aina hiyo ni kama donda linalokula mwili. Miongoni mwa hao waliofundisha hayo ni Humenayo na Fileto.[#2:17 1Tim 1:20. “Fileto” hatajwi mahali pengine isipokuwa hapa tu.]
18Hawa wamepotoka kabisa mbali na ukweli, na wanatia imani ya watu wengine katika wasiwasi kwa kusema ati ufufuo wetu umekwisha fanyika.[#2:18 1Tim 1:6; 6:21.; #2:18 Rejea 2Thes 2:2. Baadhi ya vipengele vinavyoandamana na ufufuo ni kwamba ufufuo wahusu, kwa upande mmoja, jambo la kiroho tena ni la sasa (rejea Rom 6:5-11 na Kol 2:12-13; 3:1). Lakini kipengele kingine muhimu ni kile kinachohusu kufufuliwa kweli kimwili na kwamba ni jambo linalohusu wakati ujao (1Kor 15:12-57). Humenayo na Fileto walishikilia kipengele cha kwanza na kukataa cha pili; walishikilia kwamba kwa ubatizo sisi tumekwisha fufuka na basi.]
19Lakini msingi thabiti uliowekwa na Mungu uko imara, na juu yake yameandikwa maneno haya: “Bwana anawafahamu wale walio wake,” na “Kila asemaye yeye ni wa Bwana, ni lazima aachane na uovu.”[#2:19 Jiwe la msingi ambalo lilitegemeza jengo lote liliandikwa pia jina la mwenye nyumba hiyo au jina la yule aliyeijenga.; #2:19 Hes 16:5 (kulingana na LXX); rejea Yoh 10:14-15; Rom 8:29; 1Kor 8:3.; #2:19 Ingawa nukuu hii haipatikani yote mahali pengine katika Biblia, hata hivyo inayo mambo yanayofanana na makala fulanifulani katika Biblia, kwa mfano Hes 16:26 ambayo ni sehemu ya maandishi yaleyale ambamo sentensi iliyotangulia imenukuliwa: “kuachana na uovu”, au “kuondoka kwa waovu” kunafanana.]
20Katika nyumba kubwa kuna mabakuli na vyombo vya kila namna: vingine ni vya fedha na dhahabu, vingine vya mbao na udongo, vingine vya matumizi ya heshima na vingine kwa ajili ya matumizi ya kawaida.[#2:20 Taz 2:19 maelezo. Mwandishi anaendelea na picha ya jengo ambamo kuna vyombo mbali mbali. Vyombo vya matumizi ya heshima na matumizi ya kawaida vinatajwa pia katika Rom 9:21.]
21Basi, kama mtu atajitakasa kwa kujitenga mbali na mambo hayo yote maovu, atakuwa chombo cha matumizi ya pekee, kwa sababu amewekwa wakfu, anamfaa Bwana wake na yupo tayari kwa kila kazi njema.
22Jiepushe na tamaa za ujana, fuata uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na watu wote ambao wanamwomba Bwana kwa moyo safi.[#2:22 Aya hii inafanana sana na 1Tim 6:11.]
23Epuka ubishi wa kijinga na kipumbavu; wajua kwamba hayo huleta magomvi.
24Mtumishi wa Bwana asigombane. Anapaswa kuwa mpole kwa watu wote, mwalimu mwema na mvumilivu,
25ambaye ni mpole anapowaonya wapinzani wake, kwani huenda Mungu akawajalia nafasi ya kutubu, wakapata kuujua ukweli.
26Hapo fahamu zao zitawarudia tena, wakaponyoka katika mtego wa Ibilisi aliyewanasa na kuwafanya wayatii matakwa yake.