The chat will start when you send the first message.
1Baada ya mambo haya yote kutendeka, viongozi walinijia na kunipa taarifa ifuatayo: “Watu wa Israeli, makuhani na Walawi hawajajitenga na wakazi wa nchi ambao wanatenda machukizo: Waamoni, Wamoabu na Wamisri, Wakanaani, Wahiti, Waperizi, Wayebusi na Waamori.[#9:1 Yaani, Ezra. Taz 7:27-28 maelezo.; #9:1 Haihusu hapa ubaguzi kati ya Waisraeli na watu wa mataifa hayo mengine ila, kulingana na yanayosemwa katika aya zifuatazo, kujitenga huko kulikuwa kidini (aya 21-32).; #9:1 Mataifa hayo manane yalikuwa miongoni mwa yale mataifa yaliyokuwa nchini Kanaani kabla haijanyakuliwa na Waisraeli chini ya uongozi wa Yoshua. Waisraeli walikatazwa kuoana nao (Kumb 7:1-4).]
2Wayahudi wanaoa wanawake wa kigeni na kuwaoza wavulana wao pia. Hivyo, taifa takatifu la Mungu limechanganyika na watu wa mataifa mengine Isitoshe, maofisa na wakuu ndio wa kwanza kutenda maovu hayo.”[#9:2 Kosa linalohusika ni kwamba katika ndoa za namna hiyo Waisraeli walishawishiwa kuabudu miungu ya kigeni.]
3Nilipoyasikia maelezo hayo, nilizirarua nguo zangu na joho langu, nikazing'oa nywele zangu na ndevu zangu kwa huzuni kubwa na kuketi chini kwa hofu.[#9:3 Kitendo cha kuonesha huzuni na maombolezo (Hes 14:6; Yos 7:6; Yobu 1:20; Isa 22:12).]
4Ndipo watu wote walioshikwa na hofu kwa sababu ya maneno aliyosema Mungu wa Israeli kuhusu makosa ya wale waliorudi kutoka uhamishoni walipoanza kukusanyika karibu nami hali nikikaa katika hofu hadi jioni, wakati wa kutoa tambiko.
5Jioni, wakati wa kutoa tambiko ulipofika, niliinuka mahali hapo nilipokuwa nimekaa kwa huzuni huku nguo zangu zimeraruka pamoja na joho, nikapiga magoti na kumnyoshea mikono yangu Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, na kuomba,
6nikisema, “Ee Mungu wangu, naona aibu kubwa sana kukiinua kichwa changu mbele yako. Dhambi zetu zimerundikana kupita hata vichwa vyetu; naam, makosa yetu yanafika hata mbinguni.[#9:6 Ingawa Ezra hakuwa mmoja wa hao waliooana na watu wa mataifa mengine anajiweka pamoja nao kuomba msamaha kwa Mungu. Ni kana kwamba taifa lote lilikabiliwa na dhambi hiyo ya baadhi yao.]
7Tangu nyakati za babu zetu hadi sasa, sisi watu wako tumekukosea sana. Na kwa sababu ya dhambi zetu, sisi, wafalme wetu na makuhani wetu tumetiwa mikononi mwa wafalme wa nchi za kigeni, tukauawa, tukachukuliwa mateka na kunyang'anywa mali zetu. Na hadi hivi leo, tumetiwa haya kupita kiasi.
8Lakini sasa, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kwa muda mfupi umetuonesha huruma yako na kuwawezesha baadhi yetu kuponyoka kutoka utumwani na kuishi kwa usalama mahali hapa patakatifu. Badala ya utumwa, umetupa furaha na maisha mapya.
9Hukutuacha tuishi utumwani ingawa tulikuwa tu watumwa Uliwafanya wafalme wa Persia wawe wema kwetu na kuturuhusu tuishi na kuijenga nyumba yako iliyokuwa imebomoka, ukatufanya tukae salama hapa Yuda na Yerusalemu.[#9:9 Ingawa Wapersia hawakuwatendea Waisraeli kama watumwa, hata hivyo kwa vile walikuwa kwa jumla chini yao hawakuwa na ule uhuru kamili kiutawala.]
10“Lakini sasa, ee Mungu wetu, tuseme nini baada ya hayo yote? Maana, tumeziasi amri zako
11ulizotupa kwa njia ya watumishi wako manabii ukisema: ‘Nchi mnayoiendea na ambayo itakuwa mali yenu ni nchi iliyo najisi yenye uchafu wa wakazi toka nchi mbalimbali, kwa machukizo yao, wameijaza unajisi tele kila mahali.[#9:11 Yamkini maneno haya yanatumiwa kutaja ibada kwa miungu ya uongo.]
12Kwa hiyo, msiwaoze watu hao binti zenu, wala msiwaruhusu wavulana wenu kuwaoa binti zao. Pia, msishughulikie usalama au mafanikio yao, ili nyinyi wenyewe muweze kuwa na nguvu, na mfaidi mema ya nchi hiyo na kuwaachia watoto wenu kama urithi milele.’
13Hata baada ya yote yaliyotupata kwa sababu ya maovu yetu na makosa yetu mengi, tunajua kwamba adhabu uliyotupa, ee Mungu wetu, ni ndogo ikilinganishwa na makosa yetu, na umewaacha baadhi yetu hai.
14Je, tutavunja amri zako tena na kuoana na watu hawa watendao maovu haya? Je, hutatukasirikia na kutuangamiza kabisa, asibaki hata mmoja wetu hai wala yeyote wa kutoroka?
15Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, wewe ni mwenye haki na umetuacha tubaki kama tulivyo hivi leo. Tunaungama makosa yetu mbele yako, tukijua kuwa hakuna aliye na haki yoyote ya kuja mbele yako kwa ajili ya makosa haya.”