Zaburi 29

Zaburi 29

Zaburi 29

Sauti ya Bwana wakati wa dhoruba

1Mpeni Bwana , enyi mashujaa,

mpeni Bwana utukufu na nguvu.

2Mpeni Bwana utukufu unaostahili jina lake;

mwabuduni Bwana katika uzuri wa utakatifu wake.

3Sauti ya Bwana iko juu ya maji;

Mungu wa utukufu hupiga radi,

Bwana hupiga radi juu ya maji makuu.

4Sauti ya Bwana ina nguvu;

sauti ya Bwana ni tukufu.

5Sauti ya Bwana huvunja mierezi;

Bwana huvunja vipande vipande

mierezi ya Lebanoni.

6Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama,

Sirioni urukaruke kama mwana nyati.

7Sauti ya Bwana hupiga

kwa miali ya radi.

8Sauti ya Bwana hutikisa jangwa;

Bwana hutikisa Jangwa la Kadeshi.

9Sauti ya Bwana huzalisha ayala,

na huuacha msitu wazi.

Hekaluni mwake wote wasema,

“Utukufu!”

10Bwana huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika;

Bwana ametawazwa kuwa Mfalme milele.

11Bwana huwapa watu wake nguvu;

Bwana huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.