Zaburi 81

Zaburi 81

Zaburi 81

Wimbo wa sikukuu

1Mwimbieni kwa furaha, Mungu aliye nguvu yetu;

mpigieni kelele za shangwe Mungu wa Yakobo!

2Anzeni wimbo, pigeni matari,

pigeni kinubi na zeze kwa sauti nzuri.

3Pigeni baragumu za pembe za kondoo dume

wakati wa Mwandamo wa Mwezi,

na wakati wa mwezi mpevu,

katika siku ya Sikukuu yetu;

4hii ni amri kwa Israeli,

agizo la Mungu wa Yakobo.

5Aliiweka iwe kama sheria kwa Yusufu

alipotoka dhidi ya Misri,

huko tulikosikia lugha ambayo hatukuielewa.

6Asema, “Nimeondoa mzigo mabegani mwao;

mikono yao iliwekwa huru kutoka kwa kikapu.

7Katika shida yako uliniita nami nikakuokoa,

nilikujibu katika mawingu yenye ngurumo;

nilikujaribu katika maji ya Meriba.

8“Enyi watu wangu, sikieni, nami nitawaonya:

laiti kama mngenisikiliza, ee Israeli!

9Hamtakuwa na mungu mgeni miongoni mwenu;

msimsujudie mungu wa kigeni.

10Mimi ni Bwana Mungu wako,

niliyekutoa nchi ya Misri.

Panua sana kinywa chako

nami nitakijaza.

11“Lakini watu wangu hawakunisikiliza;

Israeli hakunitii.

12Basi niliwaacha katika ukaidi wa mioyo yao

wafuate mashauri yao wenyewe.

13“Laiti watu wangu wangenisikiliza,

laiti Israeli wangefuata njia zangu,

14ningewatiisha adui zao kwa haraka,

na kuugeuza mkono wangu dhidi ya watesi wao!

15Wale wanaomchukia Bwana wangejikunyata mbele zake,

na adhabu yao ingedumu milele.

16Bali ninyi mngelishwa ngano iliyo bora,

na kuwatosheleza kwa asali inayotoka kwenye mwamba.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.