Zekaria 10

Zekaria 10

Bwana ataitunza Yuda

1Mwombeni Bwana mvua wakati wa vuli;

ndiye Bwana atengenezaye mawingu ya tufani.

Huwapa watu manyunyu ya mvua,

pia mimea ya shambani kwa ajili ya kila mtu.

2Sanamu huzungumza udanganyifu,

waaguzi huona maono ya uongo;

husimulia ndoto ambazo si za kweli,

wanatoa faraja batili.

Kwa hiyo watu wanatangatanga kama kondoo

walioteseka kwa kukosa mchungaji.

3“Hasira yangu inawaka dhidi ya wachungaji,

nami nitawaadhibu viongozi;

kwa kuwa Bwana wa majeshi

atalichunga kundi lake,

nyumba ya Yuda,

naye atawafanya kama farasi

mwenye kiburi akiwa vitani.

4Kutoka Yuda litatokea Jiwe la pembeni,

kutoka kwake vitatoka vigingi vya hema,

kutoka kwake utatoka upinde wa vita,

kutoka kwake atatoka kila mtawala.

5Kwa pamoja watakuwa kama mashujaa

wanaokanyaga barabara za matope

wakati wa vita.

Kwa sababu Bwana yu pamoja nao,

watapigana na kuwashinda wapanda farasi.

6“Nitaiimarisha nyumba ya Yuda

na kuiokoa nyumba ya Yusufu.

Nitawarejesha kwa sababu

nina huruma juu yao.

Watakuwa kama watu ambao

sijawahi kuwakataa

kwa sababu mimi ndimi Bwana Mungu wao,

nami nitawajibu.

7Waefraimu watakuwa kama mashujaa,

mioyo yao itafurahi kana kwamba ni kwa divai.

Watoto wao wataona na kufurahi,

mioyo yao itashangilia katika Bwana .

8Nitawaashiria na kuwakusanya ndani.

Hakika nitawakomboa,

nao watakuwa wengi

kama walivyokuwa mwanzoni.

9Ijapokuwa niliwatawanya miongoni mwa mataifa,

hata hivyo wakiwa katika nchi za mbali

watanikumbuka mimi.

Wao na watoto wao watanusurika katika hatari

nao watarudi.

10Nitawarudisha kutoka Misri

na kuwakusanya toka Ashuru.

Nitawaleta katika nchi ya Gileadi na Lebanoni,

na hapo hapatakuwa na nafasi ya kuwatosha.

11Watapita katika bahari ya mateso;

bahari iliyochafuka itatulizwa

na vilindi vyote vya Mto Naili vitakauka.

Kiburi cha Ashuru kitashushwa,

nayo fimbo ya utawala ya Misri itatoweka.

12Nitawaimarisha katika Bwana ,

na katika jina lake watatembea,”

asema Bwana .

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.