Sefania 3

Sefania 3

Maisha ya baadaye ya Yerusalemu

1Ole mji wa wadhalimu,

waasi na waliotiwa unajisi!

2Hautii mtu yeyote,

haukubali maonyo.

Haumtumaini Bwana ,

haukaribii karibu na Mungu wake.

3Maafisa wake ni simba wanaonguruma,

watawala wake ni mbwa-mwitu wa jioni,

ambao hawabakizi chochote

kwa ajili ya asubuhi.

4Manabii wake ni wenye kiburi,

ni wadanganyifu.

Makuhani wake hunajisi patakatifu

na kuihalifu sheria.

5Bwana aliye ndani yake ni mwenye haki,

hafanyi kosa.

Asubuhi kwa asubuhi hutoa haki yake,

kila kukipambazuka huitimiza,

bali mtu dhalimu hana aibu.

6“Nimeyaangamiza mataifa,

ngome zao zimebomolewa.

Nimeziacha barabara ukiwa,

hakuna anayepita humo.

Miji yao imeharibiwa;

hakuna mmoja atakayeachwa:

hakuna hata mmoja.

7Niliuambia huo mji,

‘Hakika utaniogopa na kukubali maonyo!’

Ndipo makao yake hayatafutiliwa mbali,

wala adhabu zangu zote hazitakuja juu yake.

Lakini walikuwa bado na shauku

kutenda kwa upotovu katika yote waliyofanya.”

8Bwana anasema,

“Kwa hiyo ningojee mimi,

siku nitakayosimama kuteka nyara.

Nimeamua kukusanya mataifa,

kukusanya falme

na kumimina ghadhabu yangu juu yao,

hasira yangu kali yote.

Dunia yote itateketezwa

kwa moto wa hasira yangu yenye wivu.

9“Ndipo nitatakasa midomo ya mataifa,

kwamba wote waweze kuliitia jina la Bwana

na kumtumikia kwa pamoja.

10Kutoka ngʼambo ya mito ya Kushi

watu wangu wanaoniabudu,

watu wangu waliotawanyika,

wataniletea sadaka.

11Siku hiyo hutaaibishwa

kwa ajili ya makosa yote uliyonitendea,

kwa sababu nitawaondoa kutoka mji huu

wale wote wanaoshangilia

katika kiburi chao.

Kamwe hutajivuna tena

katika kilima changu kitakatifu.

12Lakini nitakuachia ndani yako

wapole na wanyenyekevu,

ambao wanatumaini jina la Bwana .

13Mabaki ya Israeli hayatafanya kosa;

hawatasema uongo,

wala udanganyifu hautakuwa

katika vinywa vyao.

Watakula na kulala

wala hakuna yeyote

atakayewaogopesha.”

14Imba, ee Binti Sayuni;

paza sauti, ee Israeli!

Furahi na kushangilia kwa moyo wako wote,

ee Binti Yerusalemu!

15Bwana amekuondolea adhabu yako,

amewarudisha nyuma adui zako.

Bwana , Mfalme wa Israeli, yu pamoja nawe;

kamwe hutaogopa tena madhara yoyote.

16Katika siku hiyo watauambia Yerusalemu,

“Usiogope, ee Sayuni;

usiiache mikono yako ilegee.

17Bwana Mungu wako yu pamoja nawe,

yeye ni Shujaa mwenye nguvu anayeokoa.

Atakufurahia kwa furaha kubwa,

atakutuliza kwa pendo lake,

atakufurahia kwa kuimba.”

18“Huzuni katika sikukuu zilizoamriwa

nitaziondoa kwenu;

hizo ni mzigo na fedheha kwenu.

19Wakati huo nitawaadhibu

wote waliokudhulumu;

nitaokoa vilema na kukusanya

wale waliotawanywa.

Nitawapa sifa na heshima

katika kila nchi ambayo waliaibishwa.

20Wakati huo nitawakusanya;

wakati huo nitawaleta nyumbani.

Nitawapa sifa na heshima

miongoni mwa mataifa yote ya dunia

wakati nitakapowarudishia mateka yenu

mbele ya macho yenu hasa,”

asema Bwana .

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.