Ayubu 27

Ayubu 27

Ayubu ashikilia uelekevu wake

1Kisha Ayubu akaendelea na hoja yake, na kusema,

2Kama aishivyo Mungu, aliyeniondolea haki yangu;[#Ayu 34:5]

Huyo Mwenyezi aliyeitesa nafsi yangu;

3(Kwa kuwa uhai wangu ungali mzima ndani yangu,

Na Roho ya Mungu iko katika pua yangu;)

4Hakika midomo yangu haitanena yasiyo haki,

Wala ulimi wangu hautatamka udanganyifu.

5Hasha! Nisiwahesabie ninyi kuwa na haki;[#Ayu 13:15]

Hata nitakapokufa sitajiondolea uelekevu wangu.

6Haki yangu naishika sana, wala sitaiacha;[#Ayu 2:3; Mdo 24:16]

Moyo wangu hautanisuta wakati nikiwapo hai.

7Adui yangu na awe kama huyo mwovu,

Na mpinzani wangu awe kama asiye haki.

8Maana tumaini la mpotovu ni nini, ingawa ajipatia faida,[#Mt 16:26]

Hapo Mungu amwondoleapo roho yake?

9Je! Mungu atakisikia kilio chake,[#Mit 1:28; Isa 1:15; Mik 3:4; Zek 7:13; Yak 4:3]

Taabu zitakapomfikia?

10Je! Atajifurahisha katika Mwenyezi,[#Ayu 22:26]

Na kumlingana Mungu nyakati zote?

11Nitawafundisha ninyi mambo ya mkono wa Mungu;

Hayo yaliyo kwa Mwenyezi sitayaficha.

12Tazama, ninyi nyote mmeyaona wenyewe;

Mbona basi mmebatilika kabisa?

13Hii ndiyo sehemu ya mtu mwovu kwa Mungu,

Na urithi wa hao waoneao, waupokeao kwa Mwenyezi.

14Watoto wake wakiongezeka ni kwa upanga;[#Kum 28:32,41; Est 9:10; 2 Fal 10:6-10]

Na wazao wake hawatashiba chakula.

15Hao watakaosalia kwake watakufa kwa maradhi mabaya,[#Zab 78:64]

Wala wajane wake waliofiwa na waume hawataomboleza.

16Ajapokusanya fedha kama mavumbi,

Na kujifanyia mavazi kama udongo kwa wingi;

17Yumkini kuyatengeza, lakini wenye haki watayavaa,[#Mit 28:8; Mhu 2:26]

Nao wasio na hatia watazigawanya hizo fedha.

18Yeye hujenga nyumba yake kama mdudu,[#Omb 2:6]

Na kama kibanda afanyacho mlinzi.

19Yeye hujilaza hali ni tajiri, lakini ndio mwisho;[#Hes 20:26]

Hufunua macho yake, naye hayuko.

20Vitisho vyampata kama maji mengi;

Dhoruba humwiba usiku.

21Upepo wa mashariki humchukua, naye huondoka;

Na kumkumba atoke mahali pake.

22Kwani Mungu atamtupia asimhurumie;

Angependa kuukimbia mkono wake.

23Watu watampigia makofi,

Na kumzomea atoke mahali pake.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya