Mathayo 3

Mathayo 3

Mahubiri ya Yohana Mbatizaji

1Siku zile aliondokea Yohana Mbatizaji akihubiri katika nyika ya Yudea, na kusema,[#Mk 1:1-8; Lk 3:3-18; #Lk 1:13]

2Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.[#Mt 4:17; Mk 1:15]

3Kwa sababu huyo ndiye aliyenenwa na nabii Isaya, akisema,[#Isa 40:3; Yn 1:23]

Sauti ya mtu aliaye nyikani,

Itengenezeni njia ya Bwana,

Yanyosheni mapito yake.

4Naye Yohana mwenyewe alikuwa na vazi lake la singa za ngamia, na mshipi wa ngozi kiunoni mwake; na chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwituni.[#2 Fal 1:8]

5Ndipo walipomwendea wa Yerusalemu, na wa Yudea wote, na nchi zote za kandokando ya Yordani;

6naye akawabatiza katika mto wa Yordani, huku wakiziungama dhambi zao.

7Na alipoona wengi miongoni mwa Mafarisayo na Masadukayo wakiujia ubatizo wake, aliwaambia, Enyi wazawa wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja?[#Mt 12:34; 23:33; Mwa 3:15]

8Basi zaeni matunda yapasayo toba;

9wala msiwaze mioyoni mwenu kwamba, Tunaye baba, ndiye Abrahamu; kwa maana nawaambia ya kwamba Mungu aweza katika mawe haya kumwinulia Abrahamu watoto.[#Yn 8:33,39; Rum 2:28,29; 4:12]

10Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni.[#Mt 7:19; Lk 13:6-9; Yn 15:6]

11Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.[#Yn 1:15,26,27,33; Mdo 1:5]

12Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake; na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika.[#Mt 13:30]

Kubatizwa kwa Yesu

13Wakati huo Yesu akaja kutoka Galilaya mpaka Yordani kwa Yohana ili abatizwe.[#Mk 1:9-11; Lk 3:21-22; Yn 1:31-34]

14Lakini Yohana alitaka kumzuia, akisema, Mimi nahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu?

15Yesu akajibu akamwambia, Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote. Ndipo akakubali.

16Naye Yesu alipokwisha kubatizwa mara aliibuka kutoka majini na tazama, mbingu zikamfunukia, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua, na kutua juu yake;

17na tazama, sauti kutoka mbinguni ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.[#Mwa 22:2; Zab 2:7; Isa 42:1; Mt 12:18; 17:5; Mk 1:11; Lk 9:35]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya