Zaburi 10

Zaburi 10

Sala dhidi ya udhalimu

1Ee Mwenyezi-Mungu, mbona wasimama mbali?

Kwa nini wajificha wakati tumo taabuni?

2Kwa kiburi waovu wanawatesa maskini;

njama zao ziwanase wao wenyewe.

3Mwovu hujisifia tamaa zake mbaya,

mtu wa tamaa hulaani na kumkataa Mwenyezi-Mungu.

4Katika majivuno yake husema: “Mungu hatagundua.”

Mawazo yake yote ni: “Hakuna Mungu.”

5Njia za mwovu hufanikiwa daima;

kwake hukumu zako ziko mbali na mawazo yake,

na huwadharau maadui zake wote.

6Huwaza moyoni: “Sitakuwa na wasiwasi;

sitapatwa na dhiki maishani.”

7Kinywa chake kimejaa laana, udanganyifu na dhuluma;[#Taz Rom 3:14]

mwepesi kusema maneno ya kuchukiza na maovu.

8Hujificha vijijini huku anaotea,

amuue kwa siri mtu asiye na hatia.

Yuko macho kumvizia mnyonge;

9huotea mafichoni mwake kama simba.

Huvizia apate kuwakamata maskini;

huwanasa kwa mtego wake na kuwachukua.

10Mnyonge huvamiwa na kuangushwa chini;

huangushwa kwa ukatili wa mtu mwovu.

11Mwovu huwaza moyoni mwake: “Mungu amesahau;

ameficha uso wake, haoni kitu!”

12Inuka, ee Mwenyezi-Mungu, uwaadhibu;

usiwasahau wanaodhulumiwa.

13Ee Mungu, kwa nini mwovu anakudharau,

na kusema ati hutamfanya awajibike?

14Lakini wewe wawaona wenye dhiki na shida;

nawe daima uko tayari kuwasaidia.

Mnyonge anakutegemea wewe, ee Mungu,

wewe umekuwa daima msaada wa yatima.

15Uzivunje nguvu za mtu mwovu;

ukomeshe uovu wake wote, usiwepo tena.

16Mwenyezi-Mungu ni mfalme milele na milele!

Mataifa yasiyomjua yatatoweka nchini mwake.

17Ee Mwenyezi-Mungu, wapokea dua za mnyonge;

wampa moyo na kumtegea sikio.

18Utawatendea haki yatima na wanaodhulumiwa,

binadamu aliye udongo asiweze tena kuleta hofu.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania