Zaburi 16

Zaburi 16

Kuomba usalama

1Unilinde ee Mungu;

maana kwako nakimbilia usalama.

2Namwambia Mungu: “Wewe u Bwana wangu;

sina jema lolote ila wewe.”

3Ni bora sana hao watakatifu walioko nchini,

kukaa nao ndiyo furaha yangu.

4Lakini wanaoabudu miungu mingine,[#16:4 Maana katika Kiebrania si dhahiri.]

watapata mateso mengi.

Tambiko ya damu sitaitolea kamwe,

na majina ya miungu hiyo sitayataja.

5Wewe ee Mwenyezi-Mungu ndiwe riziki yangu kuu,

majaliwa yangu yamo mikononi mwako.

6Umenipimia sehemu nzuri sana;

naam, urithi wangu ni wa kupendeza.

7Namsifu Mwenyezi-Mungu kwa kuniongoza,

usiku dhamiri yangu yanionya.

8Namweka Mwenyezi-Mungu mbele yangu daima;[#Taz Mate 2:25-28]

yuko pamoja nami, wala sitatikisika.

9Kwa hiyo nitafurahi kwa moyo wote na kushangilia,

nami nitakaa salama salimini.

10Naam wewe hutaiacha nafsi yangu kuzimu,[#Taz Mate 13:35]

hutaniacha mimi mwaminifu wako nipate kuoza.

11Wanionesha njia ya kufikia uhai;

kuwako kwako kwanijaza furaha kamili,

katika mkono wako wa nguvu mna mema ya milele.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania