Zaburi 4

Zaburi 4

Kuomba msaada jioni

1Ee Mungu mtetezi wa haki yangu, unijibu niombapo.

Nilipokuwa katika shida, wewe ulinisaidia;

unionee huruma na kusikia sala yangu.

2Jamani, mtaniharibia jina langu mpaka lini?

Mpaka lini mtapenda upuuzi na kusema uongo?

3Jueni kuwa Mwenyezi-Mungu amejiteulia mwaminifu wake.

Mwenyezi-Mungu husikia kila ninapomwomba.

4Tetemekeni kwa hofu na msitende dhambi;[#Efe 4:26]

tafakarini vitandani mwenu na kunyamaza.

5Toeni tambiko zilizo sawa,

na kumtumainia Mwenyezi-Mungu.

6Wengi husema: “Laiti tungepata tena fanaka!

Utuangalie kwa wema, ee Mwenyezi-Mungu!”

7Lakini mimi umenijalia furaha kubwa moyoni,

kuliko ya hao walio na divai na ngano kwa wingi.

8Nalala na kupata usingizi kwa amani;

ee Mwenyezi-Mungu, wewe peke yako waniweka salama.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania