Zaburi 85

Zaburi 85

Kuliombea fanaka taifa

1Ee Mwenyezi-Mungu,

umeifadhili nchi yako;

umemjalia Yakobo bahati nzuri tena.

2Umewasamehe watu wako kosa lao;

umezifuta dhambi zao zote.

3Umeizuia ghadhabu yako yote;

umeiacha hasira yako kali.

4Uturekebishe tena, ee Mungu mwokozi wetu;

uiondoe chuki uliyo nayo juu yetu.

5Je, utatukasirikia hata milele?

Je, utadumisha ghadhabu yako kwa vizazi vyote?

6Je, hutatujalia tena maisha mapya,

ili watu wako wafurahi kwa sababu yako?

7Utuoneshe, fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu,

utujalie wokovu wako.

8Hebu nisikie anachosema Mwenyezi-Mungu;

maana anaahidi kuwapa watu wake amani,

watu wake mwenyewe wasiporudia upuuzi wao

9Hakika yu tayari kuwaokoa wanaomheshimu,

na utukufu wake utadumu nchini mwetu.

10Fadhili zake na uaminifu vitakutana;

uadilifu na amani vitaungana.

11Uaminifu utachipuka katika nchi;

uadilifu utashuka toka mbinguni.

12Naam, Mwenyezi-Mungu atatuletea fanaka,

na nchi yetu itatoa mazao yake mengi.

13Uadilifu utamtangulia Mungu

na kumtayarishia njia yake.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania