The chat will start when you send the first message.
1Ikawa baada ya siku nyingi, mnamo mwaka wa tatu wa ukame, neno hili la Mwenyezi-Mungu likamjia Elia: “Nenda ukajioneshe kwa mfalme Ahabu, halafu nitanyesha mvua nchini.”[#18:1 Yaani tangu ule ukame ulipoanza (rejea aya 1).]
2Basi, Elia akaenda kujionesha kwa Ahabu.
Wakati huo, njaa ilikuwa kali sana huko Samaria.
3Basi, Ahabu akamwita Obadia msimamizi wa ikulu. (Obadia alikuwa mtu amchaye Mwenyezi-Mungu sana,[#18:3 Katika Biblia kuna watu kadhaa wanaoitwa Obadia, lakini huyu si yule Obadia aliyekuwa mwandishi wa Kitabu cha nabii Obadia. Tunaambiwa tu alikuwa mcha Mungu na kwamba aliwathamini sana manabii wa Mwenyezi-Mungu. Lakini haisemwi kwamba yeye alikuwa nabii.]
4na wakati Yezebeli alipowaua manabii wa Mwenyezi-Mungu, Obadia aliwachukua manabii 100, akawaficha hamsinihamsini pangoni, akawa anawapelekea chakula na maji).[#18:4 Yezebeli (rejea 19:2-18). Yezebeli ndiye aliyemshawishi na kumtia moyo mfalme Ahabu awaruhusu watu wamwabudu Baali. Hao manabii wa Mwenyezi-Mungu ambao baadhi yao Yezebeli aliwaua walikuwa wakikaa katika mahali fulani fulani pa ibada na huenda walikuwa sehemu ya kundi la manabii (1Sam 10:5; 19:20; 2Fal 4:38).]
5Kisha, Ahabu akamwambia Obadia, “Labda tutapata majani na hapo tutawaokoa baadhi ya farasi na nyumbu wetu.”
6Basi, wakagawana nchi ili wapate kuipitia yote; Ahabu akaenda upande mmoja na Obadia upande mwingine.
7Obadia alipokuwa njiani, alikutana na Elia; naye Obadia alipomtambua Elia, aliinama chini na kusema, “Kumbe! Ni wewe bwana wangu Elia?”
8Elia akamwambia, “Naam! Ni mimi Elia. Nenda ukamwambie bwana wako kwamba niko hapa.”
9Obadia akasema, “Nimekosa nini hata utake kunitia hatarini ili niuawe na mfalme Ahabu?
10Nakuapia kwa jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wako aliye hai, kwamba mfalme amekuwa akikutafuta duniani kote. Na mfalme yeyote akisema kwamba hujaonekana huko, Ahabu alimtaka huyo mfalme aape na watu wake kwamba kweli hupo.
11Na sasa, wataka niende kumwambia kwamba wewe uko hapa!
12Ninahofia kwamba mara nitakapoondoka, Roho ya Mwenyezi-Mungu itakunyakua na kukupeleka mahali nisipopajua! Nikienda kumwambia Ahabu kwamba uko hapa, naye akikutafuta asikupate, ataniua mimi, ingawaje mimi mtumishi wako nimemcha Mwenyezi-Mungu tangu ujana wangu.[#18:12 Si dhahiri kwa nini Obadia anasema hivyo; lakini baadaye Elia atachukuliwa mbinguni kwa namna ya ajabu (2Fal 2:11-12). Taz pia Eze 3:12,14; 8:3; 11:1; 43:5; Mate 8:39.; #18:12 Msemo ambao Obadia anautumia kuonesha heshima kwa Elia kwani hakuwa amemfanyia chochote. Msemo huu waonesha kuwa manabii waliheshimiwa.]
13Je, huna habari kwamba Yezebeli alipokuwa akiwaua manabii wa Mwenyezi-Mungu, mimi niliwaficha manabii 100, watu hamsinihamsini pangoni, nikawa nawapa chakula na maji?
14Sasa waniambia ati niende kumwambia bwana wangu kwamba wewe Elia uko hapa! Ahabu ataniua.”
15Elia akamwambia, “Nakuapia kwa jina la Mwenyezi-Mungu wa Majeshi, aishivyo ambaye ninamtumikia: leo hii nitajitokeza mbele ya mfalme.”[#18:15 Kwa kutamka kwamba yeye Elia ni mtumishi wa Mwenyezi-Mungu anatumia sifa ambayo ilikuwa hasa ya wafalme wa Israeli ambao wadhifa wao ulikuwa kumtumikia Mwenyezi-Mungu na kuwaongoza watu wazitii amri zake lakini hawakufanya hivyo. Wadhifa wa Elia kama nabii na mtumishi wa Mungu ulikuwa kuwaongoza watu wamrudie Mwenyezi-Mungu.]
16Basi, Obadia akaenda kwa mfalme Ahabu, akampa habari hizo. Naye Ahabu akaenda kukutana na Elia.
17Ahabu alipomwona Elia, alisema, “Kumbe kweli ni wewe, mtaabishaji wa Israeli?”
18Elia akamjibu, “Mtaabishaji wa Israeli si mimi, bali ni wewe na jamaa ya baba yako. Nyinyi mmekiuka amri za Mwenyezi-Mungu na kuabudu Mabaali.
19Sasa, uwakusanye watu wote wa Israeli mbele yangu huko mlimani Karmeli. Hali kadhalika, wakusanye wale manabii 450 wa Baali, na manabii 400 wa Ashera mungu wa kike, ambao huhifadhiwa na malkia Yezebeli.”[#18:19 Mlima huu uko pwani ya Bahari ya Mediteranea karibu na upande wa magharibi wa bonde la Yezreeli.]
20Basi, Ahabu akawaita watu wote wa Israeli, akawakusanya na manabii wote kule mlimani Karmeli.
21Kisha, Elia akawakaribia watu hao, akawaambia, “Mtasitasita na kuyumbayumba mioyoni mpaka lini? Ikiwa Mwenyezi-Mungu, ndiye Mungu mfuateni; lakini ikiwa Baali ni Mungu, basi, mfuateni yeye.” Lakini watu hawakumjibu neno lolote.[#18:21 Katika ushindani huu kati ya nguvu za Baali na nguvu za Mungu, Elia anawakabili watu mara tatu kuwataka waamue: anawalaumu kwa kumwabudu Baali badala ya Mungu (18:21); atawaonesha ni nani aliye mkuu zaidi, Mungu au Baali (18:22-24) na mwishowe atawataka wawaangamize manabii wa Baali (18:39-40).]
22Hapo, Elia akawaambia, “Mimi tu ndiye peke yangu nabii wa Mwenyezi-Mungu niliyebaki, lakini manabii wa Baali wapo 450.
23Haya! Leteni fahali wawili; manabii wa Baali wajichagulie fahali mmoja, wamchinje, wamkate vipandevipande na kumweka juu ya kuni, bila kuwasha moto. Nami pia nitamtwaa huyo fahali mwingine, nitamchinja na kumweka juu ya kuni bila kuwasha moto.
24Kisha, wao watamwomba mungu wao, nami nitamwomba Mwenyezi-Mungu. Mungu atakayejibu kwa kuleta moto, huyo ndiye Mungu wa kweli.” Na hapo umati wote ukasema, “Naam! Na iwe hivyo.”
25Kisha, Elia akawaambia manabii wa Baali, “Nyinyi ni wengi; basi anzeni. Jichagulieni fahali, mtayarisheni na kumwomba mungu wenu, lakini msiwashe moto.”
26Hao manabii wakamtwaa fahali wao waliyepewa, wakamtayarisha, kisha wakaanza kumlilia Baali kutoka asubuhi hadi adhuhuri, wakirukaruka na kuyumbayumba kuizunguka madhabahu waliyotengeneza wakisema: “Ee Baali, utusikie!” Lakini hapakutokea sauti yoyote, wala hakuna aliyewajibu.
27Ilipofika saa sita mchana, Elia akaanza kuwadhihaki akisema, “Ombeni kwa sauti kubwa zaidi! Yeye ni mungu ati! Huenda ikawa amezama katika mawazo yake, amekwenda haja, au yumo safarini! Labda amelala, mnapaswa kumwamsha!”
28Manabii hao wakapiga kelele zaidi, wakajikatakata kwa visu na simi, kufuatana na desturi yao, hata wakabubujika damu.[#18:28 Kujikatakata kama sehemu mojawapo ya ibada na maombolezo ilikuwa kawaida huko Mashariki ya Kati ya Kale (taz Lawi 19:27-28; 21:5; Kumb 14:1 Hos 7:14).]
29Wakaendelea kupiga makelele na kufanya kama wendawazimu hadi alasiri wakati wa kutoa tambiko; lakini hakuna aliyewajibu wala kuwajali.
30Basi, Elia akawaambia watu, “Sogeeni karibu nami.” Wao wakamkaribia. Kisha Elia akaijenga upya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu iliyokuwa imebomolewa.
31Alitwaa mawe kumi na mawili, hesabu ya makabila kumi na mawili yaliyopewa majina ya wana wa Yakobo ambaye Mwenyezi-Mungu alimwambia “Jina lako litakuwa Israeli.”
32Kwa mawe hayo, Elia alimjengea Mwenyezi-Mungu madhabahu, akachimba na mtaro kuizunguka madhabahu hiyo; mtaro uwezao kuchukua kama debe moja na nusu la nafaka.
33Kisha akapanga kuni vizuri, akamkata vipandevipande yule fahali, akaviweka juu ya kuni. Kisha akawaambia watu, “Jazeni mitungi minne maji mkaimwagie tambiko hii ya kuteketezwa pamoja na kuni.” Wakafanya hivyo.[#18:33 Kitendo cha kumwaga maji kilikuwa na shabaha ya kuonesha ilivyo vigumu kabisa kuwasha moto hapo na hivyo kuonesha ukuu wa Mungu juu ya Baali.]
34Kisha akawaambia, “Rudieni tena.” Nao wakafanya hivyo mara ya pili. Naye akawaambia, “Fanyeni hivyo tena mara ya tatu.” Nao wakafanya hivyo.
35Maji yakatiririka chini pande zote za madhabahu, hata yakajaa mtaroni.
36Mnamo alasiri, wakati wa kutoa tambiko, nabii Elia aliikaribia madhabahu, akaomba, “Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo, waoneshe watu leo hii kwamba wewe ndiwe Mungu wa Israeli, na kwamba mimi ni mtumishi wako na nimefanya mambo haya kwa amri yako.
37Unijibu, ee Mwenyezi-Mungu; unijibu ili watu hawa wajue kuwa wewe Mwenyezi-Mungu ndiwe Mungu, na kwamba umeigeuza mioyo yao wakurudie.”
38Mara, Mwenyezi-Mungu akashusha moto, ukaiteketeza tambiko hiyo ya kuteketezwa, kuni, mawe na vumbi, na kuyakausha maji yote mtaroni.
39Watu walipoona hivyo, walianguka kifudifudi na kusema, “Mwenyezi-Mungu, ni Mungu; Mwenyezi-Mungu, ni Mungu!”
40Ndipo Elia akawaambia, “Wakamateni manabii wote wa Baali. Msimwache hata mmoja wao atoroke!” Basi, watu wakawakamata wote, naye Elia akawapeleka mtoni Kishoni, akawaulia huko.
41Baada ya hayo, Elia akamwambia mfalme Ahabu, “Nenda ukale na kunywa. Nasikia kishindo cha mvua.”[#18:41 Kwa sababu ya hiyo njaa iliyowakaba watu kutokana na ukame, watu walikuwa wanafunga kama ishara ya kumwomba Mungu aondoe baa hilo la njaa. Sasa nabii anamwambia Ahabu aende kula na kunywa kama namna ya kusema afanye sherehe kwani mwisho wa ukame unakaribia.]
42Basi, Ahabu akaenda zake kula na kunywa; naye Elia akapanda juu ya kilele cha mlima Karmeli, na huko akainama hadi chini na kuuweka uso wake katikati ya magoti yake.
43Kisha akamwambia mtumishi wake, “Sasa, nenda utazame upande wa baharini.” Mtumishi akaenda, akatazama, kisha akarudi akasema, “Hamna kitu.” Elia akamwambia, “Nenda tena mara saba.”
44Mara ya saba, huyo mtumishi akarudi, akasema, “Naona wingu dogo kama mkono wa mtu linatoka baharini.” Elia akamwambia, “Nenda umwambie mfalme Ahabu atayarishe gari lake la kukokotwa, ateremke, asije akazuiliwa na mvua.”
45Muda haukupita mrefu mbingu zikatanda mawingu mazito, upepo ukavuma, pakanyesha mvua kubwa. Ahabu naye akapanda gari lake la kukokotwa, akarudi Yezreeli.
46Nguvu ya Mwenyezi-Mungu ikamjia Elia, naye akajifunga na kukaza joho lake, akakimbia na kumtangulia Ahabu kuingia mjini Yezreeli.[#18:46 Kitendo hiki cha kutangulia ni cha mfano: kiongozi wa kweli wa watu ni nabii wa Mungu na sio mfalme Ahabu.]