Zaburi 43

Zaburi 43

Sala ya mkimbizi yaendelea

1Onesha kuwa sina hatia ee Mungu;

utetee kisa changu dhidi ya watu wabaya;

uniokoe na watu waongo na waovu.

2Nakimbilia usalama kwako ee Mungu;

kwa nini umenitupilia mbali?

Yanini niende huko na huko nikiomboleza

kwa kudhulumiwa na adui yangu?

3Upeleke mwanga na ukweli wako viniongoze,

vinipeleke kwenye mlima wako mtakatifu,

kwenye makao yako.

4Hapo, ee Mungu, nitakwenda madhabahuni pako;[#43:3-4 Maneno hayo yanagusia kitu kile kile. Hekalu lilikuwa limejengwa juu ya Mlima Siyoni. Nje ya hekalu kulikuwa na mahali pa kumtambikia Mungu. Mtunzi wa zaburi anatamka hamu yake ya kwenda huko na kumwabudu Mwenyezi-Mungu.]

nitakuja kwako, ee Mungu, furaha yangu kuu.

Nitakusifu kwa zeze, ee Mungu, Mungu wangu.

5Mbona ninahuzunika hivyo moyoni?

Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu?

Nitamtumainia Mungu,

nitamsifu tena

yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania