Zaburi 91

Zaburi 91

Mungu mlinzi wetu

1Anayekaa chini ya ulinzi wa Mungu Mkuu,[#91:1-13 Aya hizi zote zina wazo moja muhimu: ulinzi na kinga ya Mungu kwa watu wake.]

anayeishi chini ya kivuli cha Mungu Mwenye Nguvu,

2ataweza kumwambia Mwenyezi-Mungu:

“Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu;

Mungu wangu, ninayekutumainia!”

3Hakika Mungu atakuokoa katika mtego;

atakukinga na maradhi mabaya.

4Atakufunika kwa mabawa yake,[#91:4 Hapa Mwanazaburi anaeleza juu ya Mungu kwa picha au mfano wa mama ndege anavyowalinda vifaranga vyake; au kwa mfano wa wale viumbe wenye mabawa ambao walikuwa juu ya sanduku la agano na walifikiriwa kuwa ni kiti cha enzi cha Mungu.]

utapata usalama kwake;

mkono wake utakulinda na kukukinga.

5Huna haja ya kuogopa vitisho vya usiku,

wala shambulio la ghafla mchana;

6huna haja ya kuogopa baa lizukalo usiku,

wala maafa yanayotokea mchana.

7Hata watu elfu wakianguka karibu nawe,[#91:7 Hii inaweza kuwa kwa sababu ya ugonjwa au kwa vita.]

naam, elfu kumi kuliani mwako,

lakini wewe baa halitakukaribia.

8Kwa macho yako mwenyewe utaangalia,

na kuona jinsi watu waovu wanavyoadhibiwa.

9Wewe umemfanya Mwenyezi-Mungu kuwa kimbilio lako;

naam, Mungu aliye juu kuwa kinga yako.

10Kwa hiyo, hutapatwa na maafa yoyote;[#91:10 Ahadi ya Mungu siyo kwamba hakutatokea baa lolote, lile kwamba ulinzi na kinga ya Mungu utakuwako daima kama inavyodhihirika katika aya inayofuata.]

nyumba yako haitakaribiwa na baa lolote.

11Maana Mungu atawaamuru malaika zake,[#91:11 Katika Biblia malaika hutumika kama wajumbe na watumishi wa Mungu. Taz pia Malaika katika Fahirisi.]

wakulinde popote uendapo.

12Watakuchukua mikononi mwao,

usije ukajikwaa kwenye jiwe.

13Utakanyaga simba na nyoka,[#91:13 Mara nyingi wanyama hutumiwa kama mfano wa maadui. Taz Luka 10:19 na Zab 34:10.]

utawaponda wana simba na majoka.

14Mungu asema: “Nitamwokoa yule anipendaye;

nitamlinda anayenitambua!

15Akiniita, mimi nitamwitikia;

akiwa taabuni nitakuwa naye;

nitamwokoa na kumpa heshima.

16Nitamridhisha kwa maisha marefu,

nitamjalia wokovu wangu.”

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania