Kumbukumbu 9

Kumbukumbu 9

Si kwa sababu ya haki ya Waisraeli

(Kut 32:1‑35)

1Sikiliza, ee Israeli. Sasa mnakaribia kuvuka Yordani mwingie na kuwafukuza mataifa makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi pamoja na miji mikubwa yenye kuta zilizofika juu angani.

2Watu ni wenye nguvu na warefu, ni wana wa Waanaki! Mnafahamu habari zao na mmesikia inavyosemekana: “Ni nani awezaye kusimama dhidi ya Waanaki?”

3Kuweni na hakika leo kwamba Bwana Mungu wenu ndiye atakayetangulia kuvuka mbele yenu kama moto uteketezao. Atawaangamiza; atawatiisha mbele yenu. Nanyi mtawafukuza na kuwaangamiza mara moja, kama Bwana alivyowaahidi.

4Baada ya Bwana Mungu wenu kuwafukuza mbele yenu, msiseme mioyoni mwenu, “Bwana ametuleta hapa kuimiliki nchi hii kwa sababu ya haki yetu.” La, ni kwa sababu ya uovu wa mataifa haya ndio Bwana anawafukuza mbele yenu.

5Si kwa sababu ya haki yenu wala uadilifu wenu kwamba mtaimiliki nchi yao; lakini kwa sababu ya uovu wa mataifa haya, Bwana Mungu wenu atawafukuza mbele yenu, ili kutimiza lile alilowaapia baba zenu Abrahamu, Isaka na Yakobo.

6Basi mjue, si kwa sababu ya haki yenu Bwana Mungu wenu anawapa nchi hii nzuri kuimiliki, kwa kuwa ninyi ni taifa lenye shingo ngumu.

Ndama ya dhahabu

7Kumbukeni hili, kamwe msisahau jinsi mlivyomkasirisha Bwana Mungu wenu kwa hasira huko jangwani. Tangu siku mlipotoka Misri hadi mlipofika hapa, mmekuwa waasi dhidi ya Bwana .

8Kule Horebu mliamsha ghadhabu ya Bwana , kwa hiyo alikasirika sana hata akataka kuwaangamiza.

9Nilipopanda mlimani kupokea vibao vya mawe, vile vibao vya agano ambalo Bwana alilifanya nanyi, nilikaa mlimani siku arobaini usiku na mchana; sikula mkate wala sikunywa maji.

10Bwana alinipa vibao viwili vya mawe vilivyoandikwa kwa kidole cha Mungu. Juu ya vibao hivyo kulikuwa amri zote Bwana alizowatangazia kule mlimani kutoka kati ya moto siku ya kusanyiko.

11Mwisho wa siku arobaini usiku na mchana, Bwana alinipa vibao viwili vya mawe, vile vibao vya agano.

12Kisha Bwana akaniambia, “Shuka chini mara moja, kwa sababu watu wako uliowatoa katika nchi ya Misri wamepotoka. Wamegeukia mbali haraka kutoka lile nililowaagiza, wamejitengenezea sanamu ya kusubu.”

13Naye Bwana akaniambia, “Nimewaona watu hawa, nao ni watu wenye shingo ngumu sana!

14Niache, ili nipate kuwaangamiza na kufuta jina lao chini ya mbingu. Nami nitakufanya kuwa taifa lenye nguvu zaidi na kuwa wengi kuliko wao.”

15Kwa hiyo, niligeuka na kuteremka kutoka mlimani kwani mlima ulikuwa ukiwaka moto. Pia vile vibao viwili vya agano vilikuwa mikononi mwangu.

16Nilipotazama, niliona kuwa mmefanya dhambi dhidi ya Bwana Mungu wenu; mmejifanyia sanamu ya kusubu katika umbo la ndama. Mmegeuka upesi kutoka njia ile Bwana aliyowaagiza.

17Kwa hiyo nilichukua vile vibao viwili, nikavitupa na kuvipasua vipande vipande mbele ya macho yenu.

18Ndipo tena nikasujudu hadi chini mbele za Bwana kwa siku arobaini usiku na mchana. Sikula mkate wala sikunywa maji, kwa sababu ya dhambi yote mliyoifanya, mkifanya lile lililo ovu mbele za Bwana na kumkasirisha.

19Niliogopa hasira na ghadhabu ya Bwana , kwa kuwa aliwakasirikia ninyi sana na kutaka kuwaangamiza. Bali Bwana alinisikiliza tena.

20Lakini Bwana alimkasirikia Haruni kiasi cha kutaka kumwangamiza, nami wakati huo nilimwombea Haruni pia.

21Kisha nikachukua ile sanamu ya ndama mliyoitengeneza na kuichoma kwenye moto. Nikaiponda na kuisaga ikawa unga laini kama vumbi, nikatupa lile vumbi kwenye kijito kilichotiririka toka mlimani.

22Pia mlimkasirisha Bwana huko Tabera, Masa na Kibroth-Hataava.

23Vilevile wakati Bwana alipowatuma kutoka Kadesh-Barnea, alisema, “Kweeni, mkaimiliki nchi niliyowapa.” Lakini mliasi dhidi ya agizo la Bwana Mungu wenu. Hamkumtegemea wala kumtii.

24Mmekuwa waasi dhidi ya Bwana tangu nilipowajua ninyi.

25Nilianguka kifudifudi mbele za Bwana kwa zile siku arobaini usiku na mchana kwa sababu Bwana alikuwa amesema angewaangamiza ninyi.

26Nilimwomba Bwana na kusema, “Ee Bwana Mwenyezi, usiangamize watu wako, urithi wako mwenyewe ule ulioukomboa kwa uweza wako mkuu na kuwatoa katika nchi ya Misri kwa mkono wenye nguvu.

27Wakumbuke watumishi wako Abrahamu, Isaka na Yakobo. Usiangalie ukaidi wa watu hawa, uovu wao wala dhambi yao.

28Watu wa nchi ile uliyotutoa sisi wasije wakasema, ‘Ni kwa sababu Bwana hakuweza kuwachukua hadi nchi aliyokuwa amewaahidia, kwa sababu aliwachukia, akawaleta ili aje kuwaua jangwani.’

29Bali wao ni watu wako, urithi wako ule ulioutoa Misri kwa uweza wako mkuu na kwa mkono wako ulionyooka.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.