Isaya 28

Isaya 28

Ole wa Efraimu

1Ole kwa lile taji la maua, kiburi cha walevi wa Efraimu,

kwa ua linalosinyaa, uzuri wa utukufu wake,

uliowekwa kwenye kichwa cha bonde lenye rutuba:

kwa ule mji, kiburi cha wale walioshushwa na mvinyo!

2Tazama, Bwana anaye mmoja aliye na uwezo na nguvu.

Kama dhoruba ya mvua ya mawe na upepo unaoharibu,

kama mvua inayonyesha kwa nguvu na mafuriko yanayoshuka,

atakiangusha chini kwa nguvu.

3Lile taji la maua, kiburi cha walevi cha Efraimu,

kitakanyagwa chini ya nyayo.

4Lile ua linalosinyaa, uzuri wa utukufu wake,

uliowekwa kwenye kichwa cha bonde lenye rutuba,

litakuwa kama tini iliyoiva kabla ya mavuno:

mara mtu aionapo, huichuma na kuila.

5Katika siku ile, Bwana wa majeshi

atakuwa taji la utukufu,

taji zuri la maua

kwa mabaki ya watu wake.

6Atakuwa roho ya haki

kwa yeye anayeketi kwenye kiti cha hukumu,

chanzo cha nguvu

kwa wale wazuiao vita langoni.

7Hawa pia wanapepesuka kwa sababu ya mvinyo,

wanayumbayumba kwa sababu ya kileo:

Makuhani na manabii wanapepesuka kwa sababu ya kileo,

wanachanganyikiwa kwa sababu ya mvinyo;

wanapepesuka wanapoona maono,

wanajikwaa wanapotoa maamuzi.

8Meza zote zimejawa na matapishi

wala hakuna sehemu hata ndogo

isiyokuwa na uchafu.

9“Yeye anajaribu kumfundisha nani?

Yeye anamwelezea nani ujumbe wake?

Je, ni kwa watoto walioachishwa kunyonya?

Je, ni wale ambao ndipo tu wametolewa matitini?

10Kwa maana ni:

Amri juu ya amri, amri juu ya amri,

kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni;

hapa kidogo, kule kidogo.”

11Sawa kabisa, kwa midomo migeni

na kwa lugha ngeni,

Mungu atasema na watu hawa,

12wale ambao aliwaambia,

“Hapa ni mahali pa kupumzika,

waliochoka na wapumzike,”

na, “Hapa ni mahali pa mapumziko,”

lakini hawakutaka kusikiliza.

13Hivyo basi, neno la Bwana kwao litakuwa:

Amri juu ya amri, amri juu ya amri,

kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni,

hapa kidogo, kule kidogo:

ili waende na kuanguka chali,

wakijeruhiwa, wakinaswa na kukamatwa.

14Kwa hiyo sikieni neno la Bwana , enyi watu wenye dharau

mnaotawala watu hawa wa Yerusalemu.

15Ninyi mnajisifu, “Tumefanya agano na mauti,

tumefanya mapatano na Kuzimu.

Pigo linalofurika litakapopita,

haliwezi kutugusa sisi,

kwa kuwa tumefanya uongo kuwa kimbilio letu

na miungu ya uongo kuwa mahali petu pa kujificha.”

16Kwa hiyo, hili ndilo asemalo Bwana Mwenyezi:

“Tazama, ninaweka jiwe katika Sayuni,

jiwe lililojaribiwa,

jiwe la pembeni la thamani kwa ajili ya msingi thabiti.

Yeye atumainiye kamwe hatatiwa hofu.

17Nitaifanya haki kuwa kamba ya kupimia

na uadilifu kuwa timazi;

mvua ya mawe itafagia kimbilio lenu, huo uongo,

nayo maji yatafurikia mahali penu pa kujificha.

18Agano lenu na kifo litabatilishwa,

patano lenu na Kuzimu halitasimama.

Pigo linalofurika litakapowakumba,

litawaangusha chini.

19Kila mara lijapo litawachukua,

asubuhi baada ya asubuhi,

wakati wa mchana na wakati wa usiku,

litawakumba tangu mwanzo hadi mwisho.”

Kuuelewa ujumbe huu

utaleta hofu tupu.

20Kitanda ni kifupi mno kujinyoosha juu yake,

nguo ya kujifunikia ni nyembamba mno

mtu hawezi kujifunikia.

21Bwana atainuka kama alivyofanya kwenye Mlima Perasimu,

ataghadhibika kama alivyofanya katika Bonde la Gibeoni:

ili kufanya kazi yake, kazi yake ya ajabu,

ili kutimiza kazi yake, kazi yake ngeni.

22Sasa acheni dharau zenu,

la sivyo minyororo yenu itakuwa mizito zaidi.

Bwana, Bwana wa majeshi, ameniambia

habari za maangamizi yaliyoamriwa dhidi ya nchi yote.

23Sikilizeni msikie sauti yangu,

tegeni masikio na msikie niyasemayo.

24Mkulima anapolima ili apande,

je, hulima siku zote?

Je, huendelea kubomoa ardhi

na kusawazisha udongo?

25Baada ya kusawazisha shamba,

je, hatapanyi mbegu za bizari na kutawanya jira?

Je, hapandi ngano katika sehemu yake,

shayiri katika eneo lake,

na nafaka nyingine katika shamba lake?

26Mungu wake humwelekeza

na kumfundisha njia iliyo sahihi.

27Iliki haipurwi kwa nyundo,

wala gurudumu la gari halivingirishwi juu ya jira;

iliki hupurwa kwa fimbo,

na jira kwa ufito.

28Nafaka lazima isagwe ili kutengeneza mkate,

kwa hiyo mtu haendelei kuipura daima.

Ingawa huendesha magurudumu ya gari lake la kupuria juu yake,

farasi wake hawasagi.

29Haya yote pia hutoka kwa Bwana wa majeshi,

mwenye mashauri ya ajabu, na anayepita wote kwa hekima.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.