Isaya 52

Isaya 52

1Amka, amka, ee Sayuni,

jivike nguvu.

Vaa mavazi yako ya fahari,

ee Yerusalemu, mji mtakatifu.

Asiyetahiriwa na aliye najisi

hataingia kwako tena.

2Jikungʼute mavumbi yako,

inuka, uketi kwenye kiti cha utawala, ee Yerusalemu.

Jifungue minyororo iliyo shingoni mwako,

ee Binti Sayuni uliye mateka.

3Kwa kuwa hili ndilo asemalo Bwana :

“Mliuzwa pasipo malipo,

nanyi mtakombolewa bila fedha.”

4Kwa maana hili ndilo asemalo Bwana Mwenyezi:

“Hapo kwanza watu wangu walishuka Misri kuishi,

hatimaye, Ashuru wakawadhulumu.

5“Basi sasa nina nini hapa?” asema Bwana .

“Kwa kuwa watu wangu wamechukuliwa pasipo malipo,

nao wale wanaowatawala wanawadhihaki,”

asema Bwana .

“Mchana kutwa

jina langu limetukanwa bila kikomo.

6Kwa hiyo watu wangu watalijua Jina langu;

kwa hiyo katika siku ile watajua

kwamba ndimi niliyetangulia kulisema.

Naam, ni mimi.”

7Tazama jinsi miguu ya wale waletao habari njema

ilivyo mizuri juu ya milima,

wale wanaotangaza amani,

wanaoleta habari njema,

wanaotangaza wokovu,

wauambiao Sayuni,

“Mungu wako anatawala!”

8Sikiliza! Walinzi wako wanapaza sauti zao,

pamoja wanapaza sauti zao kwa furaha.

Bwana atakaporejea Sayuni,

wataliona kwa macho yao wenyewe.

9Pazeni sauti ya nyimbo za furaha pamoja,

enyi magofu ya Yerusalemu,

kwa maana Bwana amewafariji watu wake,

ameikomboa Yerusalemu.

10Mkono mtakatifu wa Bwana umefunuliwa

machoni pa mataifa yote,

nayo miisho yote ya dunia itaona

wokovu wa Mungu wetu.

11Ondokeni, ondokeni, tokeni huko!

Msiguse kitu chochote kilicho najisi!

Tokeni kati yake mwe safi,

ninyi mchukuao vyombo vya Bwana .

12Lakini hamtaondoka kwa haraka,

wala hamtaenda kwa kukimbia;

kwa maana Bwana atatangulia mbele yenu,

Mungu wa Israeli atakuwa mlinzi nyuma yenu.

Mateso na utukufu wa mtumishi

13Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa hekima;

atatukuzwa, na kuinuliwa juu, na kukwezwa sana.

14Kama walivyokuwa wengi

walioshangazwa naye,

kwani uso wake ulikuwa umeharibiwa sana

zaidi ya mtu yeyote

na umbo lake kuharibiwa

zaidi ya mfano wa mwanadamu:

15hivyo atayashangaza mataifa mengi,

nao wafalme watafunga vinywa vyao kwa sababu yake.

Kwa kuwa yale ambayo hawakuambiwa, watayaona,

nayo yale wasiyoyasikia, watayafahamu.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.