Yohana 13

Yohana 13

Yesu awanawisha wanafunzi wake miguu

1Sikukuu ya Pasaka ilikuwa imekaribia. Yesu alijua kuwa wakati wake wa kuondoka ulimwenguni ili kurudi kwa Baba umewadia. Alikuwa amewapenda watu wake waliokuwa ulimwenguni; naam, aliwapenda hadi mwisho.

2Yesu alipokuwa akila chakula cha jioni na wanafunzi wake, ibilisi alikuwa amekwisha kutia wazo la kumsaliti Yesu ndani ya moyo wa Yuda Iskariote, mwana wa Simoni.

3Yesu, akijua kwamba Baba ameweka vitu vyote chini ya mamlaka yake, na kwamba yeye alitoka kwa Mungu na alikuwa anarudi kwa Mungu,

4aliondoka chakulani, akavua vazi lake la nje, akajifunga kitambaa kiunoni.

5Kisha akamimina maji kwenye sinia na kuanza kuwanawisha wanafunzi wake miguu na kuikausha kwa kile kitambaa alichokuwa amejifunga kiunoni.

6Alipomfikia Simoni Petro, Petro akamwambia, “Bwana, je, wewe utaninawisha mimi miguu?”

7Yesu akamjibu, “Hivi sasa hutambui lile ninalofanya, lakini baadaye utaelewa.”

8Petro akamwambia, “La, wewe hutaninawisha miguu kamwe.”

Yesu akamjibu, “Kama nisipokunawisha, wewe huna sehemu nami.”

9Ndipo Simoni Petro akajibu, “Usininawishe miguu peke yake, Bwana, bali pamoja na mikono na kichwa pia!”

10Yesu akamjibu, “Mtu aliyekwisha kuoga anahitaji kunawa miguu tu, kwani mwili wake wote ni safi. Ninyi ni safi, ingawa si kila mmoja wenu.”

11Kwa kuwa yeye alijua ni nani ambaye angemsaliti, ndiyo sababu akasema si kila mmoja aliyekuwa safi.

12Alipomaliza kuwanawisha miguu yao, alivaa tena mavazi yake, akarudi alikokuwa ameketi. Akawauliza, “Je, mmeelewa nililowafanyia?

13Ninyi mnaniita mimi ‘Mwalimu’ na ‘Bwana’; hii ni sawa, maana ndivyo nilivyo.

14Kwa hiyo, ikiwa mimi niliye Bwana wenu na Mwalimu wenu nimewanawisha ninyi miguu, pia hamna budi kunawishana miguu ninyi kwa ninyi.

15Mimi nimewawekea kielelezo kwamba imewapasa kutenda kama vile nilivyowatendea ninyi.

16Amin, amin nawaambia, mtumishi si mkuu kuliko bwana wake, wala aliyetumwa si mkuu kuliko yule aliyemtuma.

17Sasa kwa kuwa mmejua mambo haya, heri kwenu mkiyatenda.

18“Sisemi hivi kuhusu ninyi nyote. Ninawajua wale niliowachagua. Lakini ni kutimiza andiko lisemalo, ‘Yeye aliyekula chakula changu ameinua kisigino chake dhidi yangu.’[#13:18 Za 41:9]

19“Ninawaambia mambo haya kabla hayajatukia, ili yatakapotukia mpate kuamini ya kuwa Mimi ndiye.

20Amin, amin nawaambia, yeyote anayempokea yule niliyemtuma anipokea mimi, naye anipokeaye mimi ampokea yeye aliyenituma mimi.”

Yesu anatabiri kusalitiwa kwake

(Mt 26:20‑25; Mk 14:17‑21; Lk 22:21‑23)

21Baada ya kusema haya, Yesu alifadhaika sana moyoni, akasema, “Amin, amin nawaambia, mmoja wenu atanisaliti.”

22Wanafunzi wake wakatazamana bila kujua kuwa alikuwa anamsema nani.

23Mmoja wa wanafunzi wake, ambaye Yesu alimpenda sana, alikuwa ameegama kifuani mwa Yesu.

24Simoni Petro akampungia mkono yule mwanafunzi, akamwambia, “Muulize anamaanisha nani.”

25Yule mwanafunzi akamwegemea Yesu, akamuuliza, “Bwana, tuambie, ni nani?”

26Yesu akajibu, “Ni yule nitakayempa hiki kipande cha mkate baada ya kukichovya kwenye bakuli.” Hivyo baada ya kukichovya kile kipande cha mkate, akampa Yuda Iskariote, mwana wa Simoni.

27Mara tu baada ya kukipokea kile kipande cha mkate, Shetani akamwingia.

Yesu akamwambia Yuda, “Lile unalotaka kulitenda, litende haraka.”

28Hakuna hata mmoja wa wale waliokuwa wameketi naye mezani aliyeelewa kwa nini Yesu alimwambia hivyo.

29Kwa kuwa Yuda alikuwa mtunza fedha, wengine walifikiri Yesu alikuwa anamwambia akanunue vitu vilivyohitajika kwa ajili ya Sikukuu, au kuwapa maskini kitu.

30Mara tu baada ya kupokea ule mkate, Yuda akatoka nje. Wakati huo ulikuwa ni usiku.

Mafundisho ya mwisho ya Bwana Yesu

Yesu atabiri kuwa Petro atamkana

(Mt 26:31‑35; Mk 14:27‑31; Lk 22:31‑34)

31Baada ya Yuda kutoka nje, Yesu akasema, “Sasa Mwana wa Adamu ametukuzwa, naye Mungu ametukuzwa ndani yake.

32Ikiwa Mungu ametukuzwa ndani ya Mwana, Mungu atamtukuza Mwana ndani yake mwenyewe, naye atamtukuza mara moja.

33“Watoto wangu, mimi bado niko pamoja nanyi kwa kitambo kidogo. Mtanitafuta, na kama vile nilivyowaambia Wayahudi, vivyo hivyo sasa nawaambia na ninyi: Niendako, ninyi hamwezi kuja.

34“Amri mpya nawapa: Mpendane. Kama mimi nilivyowapenda ninyi, vivyo hivyo nanyi mpendane.

35Mkipendana ninyi kwa ninyi kwa njia hii, watu wote watajua kuwa ninyi ni wanafunzi wangu.”

36Simoni Petro akamuuliza, “Bwana, unaenda wapi?”

Yesu akamjibu, “Ninakoenda huwezi kunifuata sasa, lakini utanifuata baadaye.”

37Petro akamuuliza tena, “Bwana, kwa nini siwezi kukufuata sasa? Mimi niko tayari kuutoa uhai wangu kwa ajili yako.”

38Yesu akamjibu, “Je, ni kweli uko tayari kuutoa uhai wako kwa ajili yangu? Amin, amin nakuambia, kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.