Yoeli 1

Yoeli 1

1Neno la Bwana ambalo lilimjia Yoeli mwana wa Pethueli.

Kuvamiwa wa nzige

2Sikilizeni hili, enyi wazee;

sikilizeni, ninyi nyote mnaoishi katika nchi.

Je, jambo kama hili lilishawahi kutokea

katika siku zenu au katika siku za babu zenu?

3Waelezeni watoto wenu,

na watoto wenu wawaambie watoto wao,

na watoto wao kwa kizazi kitakachofuata.

4Kilichosazwa na kundi la tunutu

nzige wakubwa wamekula,

kilichosazwa na nzige wakubwa

parare wamekula,

kilichosazwa na parare

madumadu wamekula.

5Amkeni, enyi walevi, mlie!

Pigeni yowe enyi wanywaji wote wa mvinyo,

pigeni yowe kwa sababu ya mvinyo mpya,

kwa kuwa mmenyangʼanywa

kutoka midomoni mwenu.

6Taifa limevamia nchi yangu,

lenye nguvu tena lisilo na idadi;

lina meno ya simba,

magego ya simba jike.

7Limeharibu mizabibu yangu

na kuangamiza mitini yangu.

Limebambua magome yake

na kuyatupilia mbali,

likayaacha matawi yake yakiwa meupe.

8Omboleza kama bikira aliyevaa gunia

akimwomboleza mume wa ujana wake.

9Sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji

zimekatiliwa mbali kutoka nyumba ya Bwana .

Makuhani wanaomboleza,

wale wanaohudumu mbele za Bwana .

10Mashamba yameharibiwa,

ardhi imekauka;

nafaka imeharibiwa,

mvinyo mpya umekauka,

mafuta yamekoma.

11Kateni tamaa, enyi wakulima,

lieni, enyi mlimao mizabibu;

huzunikeni kwa ajili ya ngano na shayiri,

kwa sababu mavuno ya shambani yameharibiwa.

12Mzabibu umekauka

na mtini umenyauka;

mkomamanga, mtende na mtofaa,

miti yote shambani, imekauka.

Hakika furaha yote ya mwanadamu

imeondoka.

Wito wa kuomboleza

13Vaeni gunia, enyi makuhani, muomboleze;

pigeni yowe, enyi mnaohudumu madhabahuni.

Njooni, vaeni gunia usiku kucha,

enyi mnaohudumu mbele za Mungu wangu;

kwa kuwa sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji

zimezuiliwa kufika katika nyumba ya Mungu wenu.

14Tangazeni saumu takatifu;

liiteni kusanyiko takatifu.

Waiteni wazee

na wote wanaoishi katika nchi

waende katika nyumba ya Bwana Mungu wenu,

wakamlilie Bwana .

15Ole kwa siku hiyo!

Kwa kuwa siku ya Bwana iko karibu;

itakuja kama uharibifu

kutoka kwa Mwenyezi.

16Je, chakula hakikukatiliwa mbali

mbele ya macho yetu:

furaha na shangwe

kutoka nyumba ya Mungu wetu?

17Mbegu zinakauka

chini ya mabonge ya udongo.

Maghala yameachwa katika uharibifu,

maghala ya nafaka yamebomolewa,

kwa maana hakuna nafaka.

18Jinsi gani ngʼombe wanavyolia!

Makundi ya mifugo yanahangaika

kwa sababu hawana malisho;

hata makundi ya kondoo yanateseka.

19Kwako, Ee Bwana , naita,

kwa kuwa moto umeteketeza

malisho ya mbugani

na miali ya moto imeunguza

miti yote shambani.

20Hata wanyama pori wanakuonea shauku;

vijito vya maji vimekauka,

na moto umeteketeza

malisho yote ya mbugani.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.