Obadia 1

Obadia 1

1Maono ya Obadia.

Hili ndilo asemalo Bwana Mwenyezi kuhusu Edomu:

Tumesikia ujumbe kutoka kwa Bwana :

Mjumbe alitumwa kwa mataifa kusema,

“Inukeni, twendeni tukapigane vita dhidi yake.”

2“Tazama, nitakufanya mdogo miongoni mwa mataifa,

utadharauliwa kabisa.

3Kiburi cha moyo wako kimekudanganya,

wewe unayeishi katika mapango ya miamba

na kufanya makao yako juu,

wewe unayejiambia mwenyewe,

‘Ni nani awezaye kunishusha chini?’

4Ingawa unapaa juu kama tai

na kufanya kiota chako kati ya nyota,

nitakushusha chini kutoka huko,”

asema Bwana .

5“Ikiwa wezi wangekuja kwako,

ikiwa wanyangʼanyi wangekujia usiku:

Lo! Tazama ni maafa kiasi gani yanakungojea:

je, si wangeiba tu kiasi ambacho wangehitaji?

Kama wachuma zabibu wangekuja kwako,

je, wasingebakiza zabibu chache?

6Lakini tazama jinsi Esau atakavyotekwa,

jinsi hazina zake zilizofichwa zitatekwa nyara!

7Wote ulioungana nao watakufukuza hadi mpakani,

rafiki zako watakudanganya na kukushinda,

wale wanaokula mkate wako watakutegea mtego,

lakini hutaweza kuugundua.

8“Katika siku hiyo,” asema Bwana ,

“je, sitaangamiza wenye hekima wa Edomu,

hao wenye ufahamu katika milima ya Esau?

9Ee Temani, mashujaa wako watatiwa hofu,

kila mmoja katika milima ya Esau

ataangushwa chini kwa kuchinjwa.

10Kwa sababu ya jeuri uliyofanya dhidi ya ndugu yako Yakobo,

aibu itakufunika;

utaangamizwa milele.

11Siku ile ulisimama mbali ukiangalia

wakati wageni walipojichukulia utajiri wake,

na watu wa nchi nyingine walipoingia malango yake

wakipiga kura kwa ajili ya Yerusalemu,

ulikuwa kama mmoja wao.

12Usingemdharau ndugu yako

katika siku ya msiba wake,

wala kufurahia juu ya watu wa Yuda

katika siku ya maangamizi yao,

wala kujigamba sana

katika siku ya taabu yao.

13Usingeingia katika malango ya watu wangu

katika siku ya maafa yao,

wala kuwadharau katika janga lao

katika siku ya maafa yao,

wala kunyangʼanya mali yao

katika siku ya maafa yao.

14Usingengoja kwenye njia panda

na kuwaua wakimbizi wao,

wala kuwatoa watu wake waliosalia

katika siku ya shida yao.

15“Siku ya Bwana iko karibu

kwa mataifa yote.

Kama ulivyotenda, nawe utatendewa vivyo hivyo,

matendo yako yatakurudia juu ya kichwa chako.

16Kama vile ulivyokunywa juu ya mlima wangu mtakatifu,

vivyo hivyo mataifa yote watakunywa mfululizo;

watakunywa na kunywa,

nao watatoweka kana kwamba hawajawahi kuwepo.

17Lakini katika Mlima Sayuni kutakuwa na wale watakaookoka;

nao utakuwa mtakatifu,

nayo nyumba ya Yakobo

itamiliki urithi wake.

18Nyumba ya Yakobo itakuwa moto,

na nyumba ya Yusufu itakuwa mwali wa moto;

nayo nyumba ya Esau itakuwa bua kavu,

nao wataiwasha moto na kuiteketeza.

Hakutakuwa na watakaosalimika

kutoka nyumba ya Esau.”

Bwana amesema.

19Watu kutoka nchi ya Negebu

wataimiliki milima ya Esau,

na watu kutoka Shefela

wataimiliki nchi ya Wafilisti.

Watayamiliki mashamba ya Efraimu na Samaria,

naye Benyamini atamiliki Gileadi.

20Kundi la Waisraeli walio uhamishoni Kanaani

watarudi na kuimiliki nchi hadi Sarepta.

Walio uhamishoni Sefaradi kutoka Yerusalemu

wataimiliki miji ya Negebu.

21Waokoaji watakwea juu ya Mlima Sayuni

kutawala milima ya Esau.

Nao ufalme utakuwa wa Bwana .

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.