Zaburi 58

Zaburi 58

Zaburi 58

Mungu kuwaadhibu waovu

1Enyi watawala, je, kweli mwanena kwa haki?

Je, mnahukumu kwa unyofu miongoni mwa watu?

2La, mioyoni mwenu mnatunga udhalimu,

na mikono yenu hueneza jeuri duniani.

3Waovu ni wapotovu tangu kuzaliwa kwao,

toka tumboni mwa mama zao

ni wakaidi na husema uongo.

4Sumu yao ni kama sumu ya nyoka,

kama ile ya fira ambaye ameziba masikio yake,

5ambaye hatasikia sauti ya kutumbuiza ya mwaguzi,

hata kama mganga angecheza kwa ustadi kiasi gani.

6Ee Mungu, yavunje meno katika vinywa vyao;

Ee Bwana , vunja meno makali ya hao simba!

7Na watoweke kama maji yanavyotiririka;

wanapovuta pinde zao, mishale yao na iwe butu.

8Na wawe kama konokono anayeyeyuka akitembea,

kama mtoto aliyezaliwa akiwa mfu.

9Kabla vyungu vyenu havijapata moto wa kuni za miiba,

zikiwa mbichi au kavu,

waovu watakuwa

wamefagiliwa mbali.

10Wenye haki watafurahi wakilipizwa kisasi,

watakapochovya nyayo zao katika damu ya waovu.

11Ndipo wanadamu watasema,

“Hakika utulivu wa wenye haki bado una thawabu,

hakika kuna Mungu ahukumuye dunia.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.